Rais Magufuli - Huyu ndiye Mkuu wa Mkoa kinara anayepiga kazi hana mfano


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, amemtaja mkuu wa mkoa wa Simiyu Mh. Anthony Mtaka, kuwa ndiye mkuu wa mkoa kinara anayepiga kazi na kwamba hana mfano licha ya kupuuzwa kabla  hajamteua.

Hayo ameyasema leo mkoani Simiyu wakati akihutubia wananchi wa mkoa huo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jioni hii ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku 7 katika mikoa ya kanda ya ziwa.

Rais Magufuli ameeleza kuwa, wakati anajaribu kutafuta wakuu wa Wilaya na wakuu wa mikoa aliambiwa na vyombo vyake kuwa Mtaka hafai hata U-DC lakini yeye akaamua kumteua kuwa mkuu wa mkoa kwasababu anajua watu wazuri huwa wanapigwa vita sana.

''Nilipotaka kumteua niliuliza vyombo vyangu nikaambiwa hafai kabisa lakini nimeuliza ripoti ya Wakuu wa Mikoa wanaofanya kazi vizuri, wakaniletea Mtaka ndio namba moja na namba mbili ni yeye kwa kifupi hana mfano'', amesema.

Aidha Rais Magufuli ambaye atakamilisha ziara yake katika mikoa hiyo siku ya Jumatatu Septemba 10, 2018 amemtaka Mtaka kuendelea kuchapa kazi wala asiyumbishwe kwasababu yeye anajua watu wanaopigwa vita na kuwekewa maneno ya ajabu ndio wazuri.

Comments

Popular posts from this blog