Maafisa Ugavi Waaswa Kuzingatia Sheria na Kanuni Katika Manunuzi

Maafisa Ugavi Wametakiwa Kuzingatia Sheria Kanuni na Taratibu za Manunuzi ili kuleta thamani halisi ya fedha zinazotumika katika sekta hiyo ili halmashauri zote zitekeleze dhana ya kutoa huduma bora kwa wananchi.
Akizungumza wakati akifungua mafunzo kwa maafisa hao leo Jijini Mbeya, Mkurugenzi msaidizi anayeshughulikia shughuli za Serikali, Idara ya Tawala za Mikoa Bw. Johnson Nyingi amewata  kuzingatia weledi na taratibu zote zinazosimamia sekta ya manunuzi kwa kuzingatia mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 yanayoendelea kwa mikoa ya Mbeya, Rukwa, Njombe na Songwe.

1
Mkurugenzi msaidizi anayeshughulikia shughuli za Serikali, Idara ya Tawala za Mikoa Bw. Johnson Nyingi akifungua mafunzo kwa maafisa ugavi wa mikoa ya Mbeya, Njombe, Rukwa na Songwe leo Jijini Mbeya.

Mafunzo hayo yanaendeshwa na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)  kwa ufadhili wa Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) na kutekelezwa kupitia  mradi wa uimarishaji wa mifumo ya sekta za umma (PS3). Mradi huu ni wa miaka mitano na unatekelezwa katika mikoa 13 ya Tanzania bara.
“ Mafunzo haya yanalenga kuwajengea uwezo maafisa ugavi ili kuongeza tija katika huduma mnazotoa kwa wananchi, mifumo ipo ili kuwezesha utendaji wenu uwe na tija kwa wale mnaowahudumia” Alisisitiza Bw. Nyingi
Akifafanua amesema kuwa washiriki wanalo jukumu la kushauri viongozi wao katika maeneo yao juu ya namna bora yakutumia rasilimali fedha wakati wa kufanya manunuzi yanayolenga kuwasaidia wananchi kupata maendeleo endelevu .
Aliongeza kuwa mafunzo kwa maafisa ugavi hao yamekuja wakati muafaka ambapo Serikali ya Awamu ya Tano imeweka kipaumbele katika usimamizi wa rasilimali fedha katika halmashuri zote ili ziweze kuwanufaisha wananchi wote.
“ Zaidi ya asilimia 70 ya fedha za Serikali zinatumika katika manunuzi hivyo jukumu la maafisa ugavi ni kuhakikisha kuwa sheria na taratibu zote za manunuzi zinazingatiwa kikamilifu” Alisisitiza Bw. Nyingi.

2
Afisa Ugavi Kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga Bw. Martin Sanane ambaye alikuwa Mwenyekiti wa mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 yanayowashirikisha  Maafisa Ugavi wa mikoa ya Mbeya, Njombe, Rukwa na Songwe yanayofanyika kwa siku mbili kuanzia leo Jijini Mbeya .

Kwa upande wake mmoja wa wawezeshaji wa mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ( TAMISEMI) Bw. Allan Bendera amesema kuwa jambo la muhimu kwa maafisa ugavi pamoja na mafunzo ya matumizi ya mfumo huo ni kuwa wazalendo katika kutekeleza majukumu yao kwa maslahi ya Taifa.
Aliongeza kuwa jukumu la maafisa ugavi ni chachu katika kuchochea maendeleo katika halmashauri zote hapa nchini.
Pia aliwaasa washiriki wa mafunzo hayo kuzingatia yale watakayojifunza ili yaweze kuwanufaisha wale ambao hawakushiriki katika mafunzo hayo.


3
Mkurugenzi msaidizi anayeshughulikia shughuli za Serikali, Idara ya Tawala za Mikoa Bw. Johnson Nyingi akisisitiza umuhimu wa maafisa manunuzi katika kuleta tija kwa huduma zinazotolewa kwa wananchi.
4
Kiongozi wa Timu ya Habari na Mawasiliano PS3 Bi. Leah Mwainyekule akifurahia jambo na Mshauri wa mifumo ya fedha wa PS3 Bw. Ramadhani Mseya (katikati) na Meneja Mradi wa PS3 mkoa wa Rukwa Bi. Rose Mangilima (kushoto) .
5
Mkurugenzi msaidizi anayeshughulikia shughuli za Serikali, Idara ya Tawala za Mikoa Bw. Johnson Nyingi (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya washiriki wa mafunzo  ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 ambao ni maafisa ugavi wa mikoa ya Mbeya, Njombe, Rukwa na Songwe leo Jijini Mbeya.
6
Mkurugenzi msaidizi anayeshughulikia shughuli za Serikali, Idara ya Tawala za Mikoa Bw. Johnson Nyingi akifurahia jambo na  wawezeshaji wa mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 kutoka Ofisi ya Rais , Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ambao ni  mchumi kutoka Idara ya Sera na Mipango Bw. Allan Bendera (kulia) na Afisa Usimamizi Fedha Bw. Mmaka Mwinjaka (katikati) leo Jijini Mbeya mara baada ya kufungua mafunzo hayo yaliyowashirikisha maafisa ugavi wa mikoa ya Njombe, Rukwa, Mbeya na Songwe.
7 

8
Sehemu ya Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi wakati wa mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 yaliyowashirikisha maafisa ugavi wa mikoa ya Njombe, Rukwa, Mbeya na Songwe leo Jijini Mbeya.
9
Mwezeshaji wa mafunzo ya matumizi ya mfumo wa Epicor 10.2 kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ( TAMISEMI) Bw. Allan Bendera akisisitiza umuhimu wa maafisa ugavi kuzingatia uzalendo katika kutekeleza majukumu yao wakati akiwasilisha mada kwa maafisa ugavi wa mikoa ya Njombe, Rukwa, Mbeya na Songwe leo Jijini Mbeya   kuhusu mfumo wa Epicor 10.2 leo Jijini Mbeya.
(Picha zote na Frank Mvungi- MAELEZO, Mbeya

Comments

Popular posts from this blog