Halima Mdee Akamatwa na Polisi Akitokea Afrika Kusini


Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee.
Jeshi la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam limemkamata Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee.
Mdee amekamatwa leo alfajiri uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere akitokea nchini Afrika Kusini inakoelezwa alilazwa kwa matibabu.
Meya wa Ubungo, Boniface Jacob amethibitisha kukamatwa kwa Halima Mdee ambapo amesema; “Ni kweli amekamatwa leo Saa 9 alfajiri Airport, akitokea Afrika Kusini alipokuwa amelazwa kwa matibabu na sasa yupo Central.”
Mdee ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) huenda akaunganishwa na vigogo wengine sita akiwamo Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe katika kesi inayowakabili.
Vigogo hao wengine tayari wamekwisha kupandishwa kizimbani katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu, Dar es Salaam na kusomewa mashtaka nane.
Kukamatwa kwa Mdee kunafikisha watuhumiwa saba kati ya nane ambao wamekwisha kuhojiwa mwingine ambaye bado na huenda anatafutwa na jeshi hilo ni mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche.
UPDATE
Mpaka mchana wa leo tarehe 01/03/2018, Jeshi la Polisi wameendelea kumshikilia Mhe Halima Mdee (Mb), katika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es salaam na hajapatiwa dhamana pamoja na Daktari wake kuwathibitishia polisi kuwa ni mgonjwa

Comments

Popular posts from this blog