Mkurugenzi wa TBC, Dkt. Ayub Rioba Apata Ajali Kigoma


Gari alilokuwa akilitumia Mkurugenzi wa TBC baada ya kupata ajali.

Watu wawili wamefariki dunia wilayani Kasulu mkoani Kigoma kufuatia ajali ya gari la Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Dkt. Ayub Rioba, lililokuwa likitokea wilayani Kibondo kwenda Kigoma mjini jana.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Kigoma, Kamishna Msaidizi Martin Otieno amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema kuwa chanzo ni utelezi uliosababisha gari kuacha njia na kuwagonga waenda kwa miguu watatu.
Mkurugenzi wa TBC, Ayoub Rioba (kushoto) akiwa katika eneo la ajali na watu wengine.
Kamanda Otieno aliwataja waliofariki katika ajali hiyo kuwa ni Teresia Mpoma (55) mkulima na mkazi wa Nyakitonto, Yuster Masharubu (55) mkazi wa Nyakitonto na majeruhi mmoja, Diana Shedrack (10) mwanafunzi shule ya Msingi Nyakitonto, ambaye hali yake ilielezwa kuwa mbaya huku akiendelea na matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Kasulu.

Amesema gari hilo lenye namba za usajili STK 8769 lilikuwa na abiria wawili akiwemo Dkt. Rioba na Mkuu wa Kanda ya Magharibi wa TBC Mhandisi Zebron Mafuru ambao wote walitoka salama na hali zao ni nzuri.

Kamanda Otieno aliongeza kuwa  utelezi huo uliotokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika mkoa huo, hivyo amewaomba madereva kuendesha kwa umakini kutokana na ubovu wa barabara hiyo na kuzingatia sheria za barabarani.

Dkt. Rioba yuko katika ziara ya kukagua vituo vipya vya matangazo vilivyojengwa katika maeneo ya mipakani.

Comments

Popular posts from this blog