Madiwani watatu Chadema wahamia CCM

 Chadema katika Halmashauri ya Tunduma, wilaya ya Momba mkoani Mbeya kimepata pigo baada ya madiwani wake watatu kuhamia CCM.

Madiwani hao na kata zao katika mabano ni Ayub Mlimba (Mwaka Kati), Simon Mbukwa (Kaloleni) na Amos Nzunda (Mpemba) na walitambulishwa jana mchana katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na Mkuu wa Wilaya ya Momba, Jumaa Irando.

Wakizungumza na Mwananchi madiwani hao waliohamia CCM wamesema wamechukua uamuzi huo baada ya kuona Chadema kimepoteza mwelekeo Tunduma, huku viongozi wake wakitoa amri za kibabe wakitaka wanachama kutozungumza chochote.

“Unajua baraza la madiwani Tunduma linaundwa na Chadema, sasa tunapewa maagizo ya nini cha kuzungumza na kusimamia hata kama hayaendani na mahitaji ya wananchi wetu kwa lengo tu la watu wachache ndani ya chama,” alisema Nzunda.

Mlimba alisema sababu ya kuhamia CCM ni kufurahishwa na utendaji kazi wa Rais John Magufuli huku Mbukwa akieleza sababu yake kuondoa Chadema kuwa ni mvutano na mtafaruku uliokikumba chama hicho.

“Tulichokuwa tunakipigania sasa kinatekelezwa na Serikali iliyopo madarakani. Pia suala la kupingwa kila unapozungumzia jitihada za Serikali sikupenda,” alisema Mbukwa.

Akizungumzia kujiuzulu uanachama kwa madiwani hao, mwenyekiti wa Chadema Jimbo la Tunduma, Boniface Mwakabanje alisema ataitisha kikao cha dharura cha madiwani wote wa chama hicho jimboni humo. “Hata hivyo, madai waliyotoa hao kuwa kuna mvutano ndani ya Chadema si kweli,” alisema.

Wamkataa msimamizi Kinondoni

Siku 10 kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa ubunge Jimbo la Kinondoni, Chadema kimeibuka na kumkataa msimamizi wa uchaguzi huo, Aron Kagurumjuli kwa madai kuwa ameshindwa kusimamia taratibu za uchaguzi.

Pia, chama hicho kikuu cha upinzani nchini kimemwandikia barua Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) wakiituhumu CCM kuandaa mikakati ya kufanya vurugu siku ya uchaguzi huo, Februari 17.

Hayo yameelezwa jana na Mkurugenzi wa Operesheni na Mafunzo wa Chadema, Benson Kigaila katika mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Katika maelezo yake Kigaila alidai kuwa CCM imeandaa vikundi vya watu, silaha kwa ajili ya kufanya vurugu katika uchaguzi huo na kuomba NEC na Polisi kuhakikisha unakuwa huru.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Kate Kamba alijibu tuhuma hizo akisema, “Si kweli hakuna kijana wala mwanachama wa CCM anayefanya hivyo. Tunafanya kampeni za kistaarabu na kila kinachofanyika kwenye uchaguzi ni cha kistaarabu. Wao ndio wanayafanya haya halafu wanatugeuzia sisi.”

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM), Kheri James alidai kuwa Chadema kimekodi vijana kutoka Tarime na Kilimanjaro na kwamba wamepanga kupambana na wanachama wa CCM.

“Polisi kama hawajui sisi tunajua na wakitaka kuamini tunajua tutaweka hadharani silaha zao na wanachopanga kukifanya. Wanajihami ili wakifanya ionekane walisema. Watambue kuwa tunafahamu kila wanachofanya, walikofikia na mipango yao. Hawana jipya zaidi ya kusubiri tuwaumbue,” alisema James.

Katika maelezo yake, Kigaila alisema mwenendo wa uchaguzi, hasa kamati ya maadili ya Kinondoni inayoongozwa na Kagurumjuli inasimamia mambo yasiyoihusu.

Alisema malalamiko yanayotolewa ni ya kijinai na hayawezi kufanyiwa kazi na kamati hiyo, “Kimsingi kamati ya maadili haina uwezo nayo, yanapaswa kupelekwa polisi yenye jukumu ya kufanya uchunguzi.

“Watu wakipiga, wakipigwa wanashughulikiwa na polisi. Mkurugenzi ni msimamizi wa uchaguzi lakini amekuwa akiyashughulikia kinyume cha kanuni,” alisema.

Alisema katika barua hiyo, wameeleza mienendo ya mkurugenzi huyo wakidai kuwa si mizuri, “Hatumkubali, hatumtaki, aondolewe na tunapinga kwani hawezi kutenda haki.”

Alibainisha kuwa suala la jinai ambalo Kagurumjuli analishughulikia ni la madai ya mwanachama wa CCM kupigwa ma vijana wa Chadema, “Hatujajua hao vijana wanaotuhumiwa ni wa Chadema au la, lakini hata kama ni kweli, mwanachama mmoja huwezi kuiwajibisha Chadema.”

Katika mkutano huo, Kigaila alidai kuwa CCM imeanza kuandaa vijana kufanya vurugu katika uchaguzi huo na kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuchukua hatua.

“Tumeandika barua kwa IGP na NEC. Tumesema yeyote atakayejeruhiwa CCM iwajibike kwani imeanza kusambaza silaha, mashoka, nondo na mapanga.”

Mwenyekiti wa Kamati ya Operesheni ya Kampeni Kinondoni, Frederick Sumaye alisema ana imani kwamba tuhuma hizo zitafanyiwa kazi.

Waziri Mkuu huyo wa zamani alisema jitihada kubwa zinapaswa kufanyika nchini ili Taifa kutoondolewa katika mfumo wa vyama vingi kwa madai kuwa vyombo vinavyosimamia uchaguzi vinahakikisha wapinzani haushindi.

“Tunaitaka NEC katika chaguzi hizi itende haki, Polisi wanaosimamia amani wote watende haki ili uchaguzi ufanyike kwa amani. Wasimamizi wa uchaguzi watende haki,” alisema Sumaye.

Kampeni zaendelea

Katika kampeni za uchaguzi za CCM jimbo la Kinondoni zilizofanyika Tandale kwa Tumbo, mgombea wa chama hicho, Maulid Mtulia aliahidi kujenga barabara ya Mkundube kupitia Manjunju, kwamba ikikamilika itaanzishwa safari mpya ya mabasi kutoka Tandale-Mbagala na Tandale- Muhimbili.

Mtulia aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CUF, kabla ya kuhamia CCM ambako alipitishwa tena kugombea nafasi hiyo alisema, “Hakuna chama imara kama CCM ndiyo maana nikajiunga nacho. Najua matatizo yenu ni shule na soko, kuna fedha za ujenzi wa Soko la Tandale zimetengwa.

“Katika kusaidia vijana, tutatoa pikipiki za mikopo ili waendelee na kazi na kulipa kidogokidogo badala ya kuwakopesha Sh50,000 ambazo haziwasaidii chochote.”

Akizungumza katika mkutano wa kampeni wa Chadema jimboni humo uliofanyika Kigogo Mbuyuni, mgombea wa chama hicho, Salum Mwalimu alisema atawatumikia wakazi wa Kinondoni bila kujali itikadi zao.

“Kina mama wa Kinondoni siwezi kuwasahau nitakwenda kuwatetea hasa kuhusu upatikanaji wa mikopo. Polisi sijawasahau nikiwa mbunge nitakwenda kupigania maeneo yenu ya kazi ili yawe katika hali nzuri. Najua umuhimu wenu niliwatetea tangu nikiwa mtangazaji wa televisheni ya Channel 10,” alisema.

Mgombea wa CUF Kinondoni, Rajabu Salum alisema akiwa mbunge, atahakikisha anaweka kipaumbele kwenye elimu, afya na ajira.

“Nitahakikisha wanafunzi wanakula shuleni ili waweze kufanya vizuri kwenye masomo. Nitahakikisha waendesha bodaboda wanakuwa na vikundi vilivyosajiliwa na kuwatafutia mwanasheria ili wasisumbuliwe. Pia nitaimarisha michezo,” alisema.

Siha kwachafuka

Jana, katika Wilaya ya Siha Mkoa wa Kilimanjaro Polisi walilazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi wa Kijiji cha Ngarenairobi waliodaiwa kufanya maandamano bila kuwa na kibali.

Wananchi hao walikuwa wakiandamana kushangilia kuachiwa kwa dhamana kwa mwenyekiti wa Chadema katika kijiji hicho, Stanley Nkini ambaye alikamatwa na wenzake wawili kwa tuhuma za wizi wa kutumia silaha na shambulio.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Koka Moita alisema walitumia mabomu hayo kuwatawanya wananchi kwa sababu maandamano yao yangesababisha uvunjifu wa amani.

Katika uchaguzi wa ubunge Jimbo la Siha, mgombea wa Chadema, Elvis Mosi anachuana vikali na mgombea wa CCM, Dk Godwin Mollel ambaye awali, alikuwa mbunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya Chadema, kabla ya kujiuzulu na kujiunga na chama tawala.

Comments

Popular posts from this blog