Mbunge Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ Aitwa Polisi


MBUNGE wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu kama ‘Sugu’ na mratibu wa chama hicho Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Emmanuel Masonga wameitwa katika Kituo Kikuu cha Polisi mkoani humo huku wakisema hawajui sababu ya wito huo.
Wawili hao wamesema wanahisi wito huo unatokana na mkutano wa hadhara alioitisha mbunge huyo katika Viwanja vya Shule ya Msingi Mwenge jijini Mbeya.

Sugu amesema leo Jumanne kuwa, juzi jioni alipigiwa simu na Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Mbeya (RCO) kwamba yeye na Masonga wafike jana ofisini kwa ajili ya mazungumzo lakini alimueleza kuwa itakuwa ni siku ya sikukuu hivyo itakuwa vigumu ngumu kwenda, hivyo walikubaliana wafike leo.
“Polisi walinipigia simu juzi jioni wakinitaka mimi na Masonga twende Makao Makuu ya Polisi jana, nikawaambia itakuwa ni sikukuu hivyo tukakubaliana leo asubuhi. Sasa hivi tupo njiani tunaelekea huko kuitika wito. Sijajua sababu, lakini nadhani ni uchochezi,” amesema Sugu.

Masonga amesema anaamini sababu ya kuitwa kwao inatokana na mkutano wao wa hivi karibuni na wananchi ambapo Masonga ndiye aliyemkaribisha Sugu kuzungumza na wananchi na alifunga mkutano, lakini kabla ya kumkaribisha alizungumza machache.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Mohammed Mpinga hajazungumzia wito huo.

Comments

Popular posts from this blog