MAMA ALIA… NATESEKA ZAIDI YA WASTARA

Staa wa filamu za Kibongo, Wastara Juma.

Hujafa hujaumbika! Wakati staa wa filamu za Kibongo, Wastara Juma akiendelea kuomba michango kwa Watanzania ili akatibiwe mguu nchini India, mama mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Sidonia Ntabashigwa mkazi wa Salasala jijini Dar yupo hoi kitandani akisema, anaamini mateso anayopata ni makubwa mno kuliko hata ya msanii huyo.
Mguu wa Bi. Sidonia Ntabashigwa uliokatwa.
Akizungumza na Amani mama huyo alisema, anateseka kitandani kwa miaka miwili sasa na hawezi kutembea kwani mguu mmoja umevunjika na mwingine viungo vimehama sehemu yake.
Mama huyo anaeleza kuwa, miaka miwili iliyopita akiwa katika stendi ya daladala Mbuyuni, Tegeta Dar, gari liliacha njia na kumgonga, ambapo alivunjika mguu ambao baadaye ulikatwa kwenye eneo la juu ya goti huku mguu mwingine ukiwa umegeuka yaani viungo vyake vikahama sehemu yake halisi.

Mguu wa Wastara uliokatwa.

“Sikuwa ni hili wala lile, nimejikalia kituoni nasubiri daladala ndipo ghafla nikashangaa gari limekuja kunigonga na baada ya hapo sikujitambua tena hadi nilipojikuta hospitali,” alisema mama huyo ambaye anaishi kwenye chumba kimoja akiwa na wanaye sita.

Mama huyo kwa masikitiko alieleza kwamba, alilazwa kwa muda mrefu kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili na baadaye aliruhusiwa kurudi nyumbani akapewa magongo ya kutembelea, lakini hawezi kuyatembelea kwa sababu mguu mwingine bado una tatizo kubwa.
Mguu mwingine wa Sidonia Ntabashigwa.

“Nateseka sana yaani mateso yangu ni zaidi ya Wastara kwani siwezi kutembea wala kufanya kitu chochote.
“Hapa nina watoto sita, tunaishi kwenye chumba hiki kimoja pamoja na baba yao ambaye hana kazi, yaani hata choo chenyewe ni mpaka tukaombe kwa jirani, nina mateso makubwa sana jamani,” alisema mama huyo na kuongeza:

“Mimi naweza kusema haya mateso ninayoyapata yanazidi hata ya Wastara maana nimesoma kwamba yeye angalau hata aliweza kuwekewa huo mguu wa bandia, akawa anaendelea na shughuli zake za kila siku.

…Akiwa amejilaza.

“Mimi hapa kama unavyoniona. Sina mguu wa bandia, siwezi kufanya shughuli za kila siku. Hapa kama unavyoniona ni mtu wa kujilaza tu katika hiki kigodoro changu,” alisema mama huyo.

Mama huyo aliendelea kueleza kuwa pamoja na mateso hayo bado mguu mmoja anatakiwa kufanyiwa upasuaji ili kurekebisha viungo, lakini amekosa fedha zinazotakiwa shilingi milioni moja.

Kutokana na mateso yake mama huyu anawaomba watanzania wote walioguswa na mateso aliyonayo wamsaidie kwa chochote walichonacho.

Kutoa ni moyo na si utajiri, kama umeguswa na mateso ya huyu mama na una chochote cha kumsaidia wasiliana naye kwa namba 0653659379.
Stori: Gladness Mallya na Erick Evarist

Comments

Popular posts from this blog