Jaji Warioba ashauri Viongozi wakutane na Wazungumze

Waziri Mkuu wa zamani, Joseph Warioba amewataka viongozi wa kisiasa kujenga utamaduni wa kukutana wanapogundua kuna matukio yanayoashiria uvunjifu wa amani.
Jaji Warioba ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba amesema waasisi wa Taifa walijenga umoja na misingi ya maendeleo ambayo kuna dalili ya kutoweka.
Amesema hayo leo Alhamisi Oktoba 26,2017  jijini Dar es Salaam akifungua mdahalo wa mashauriano juu ya kuhamasisha, kusisitiza, kulinda na kudumisha amani, umoja na maridhiano nchini.
Amesema viongozi wa dini wamekuwa na kawaida ya kukutana wanapoona mambo hayaendi sawa jambo ambalo ni zuri na linapaswa kuendelea.
Jaji Warioba amesema kuna viashiria vya kutoweka kwa amani na viongozi wa kiserikali na kisiasa wanapaswa kuiga kile wanachofanya wenzao wa dini.
"Amani ikitoweka kuirudisha ni shida au kuiendeleza. Viongozi hasa hawa wa kisiasa wawe wepesi kukutana na kuzungumza, tuache malumbano na hasa viongozi wa kisiasa na tukiendelea wanaweza kutufikisha pabaya," amesema Jaji Warioba.
Amesema ,"Hata kama wanatumia mitandao ya kijamii au vyombo vya habari kujibizana ni muhimu viongozi wa kisiasa wawe tayari kukutana kama wanavyofanya viongozi wa dini."
Jaji Warioba amesema, ''Nchi haiwezi kuendeleshwa kwa huyu kuongea hiki, huyu naye anamjibu kupitia vyombo vya habari. Hapana, hawa watu wakae wazungumze."
Amesema Watanzania wanapaswa wakae pamoja, waone matatizo na kuyazungumza na wafikie muafaka kwa kuwa hakuna njia nyingine ni kukaa na kuzungumza.
"Tunayo matatizo katika nchi yetu, hawa viongozi wa kisiasa lazima wakutane wazungumze na kikao hiki tujadili hapa na tupeleke ujumbe wetu kwa wote wanaohusika kwa lengo la kudumisha amani yetu," amesema.
Awali, akisoma hotuba ya Mkurugenzi wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF), Joseph Butiku aliye nje ya nchi, Miraji Magai amesema lengo la kikao ni kutafakari kwa makini unyenyekevu, uhuru na uwazi wa kiwango cha kutosha, nyufa ndogo au viashiria vinavyoweza kulegeza au kuashiria kuvunja amani na umoja wa Taifa.
"Vipo viashiria vinavyoweza kutuvunjia umoja na amani yetu. Tutumie kikao hiki kuvitambua na kukubali kwamba vipo, hivyo tukitafakari kwa makini vyanzo au asili ya viashiria hivyo," amesema.
Mbali ya Magai, Msaidizi Maalumu wa Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Gallus Abeid amesema kabla ya kuandaa mdahalo huo walikwenda katika mikoa na kuzungumza na makundi na viongozi wa kiserikali kuhusu matatizo yaliyotokea na jinsi ya kuyapatia ufumbuzi.
Chanzo: Mwananchi

Comments

Popular posts from this blog