Katibu Mkuu Chadema Ahojiwa Kuhusu ‘Watu Wasiojulikana’

Dk Vincent Mashinji.
KATIBU Mkuu wa Chadema, Dk Vincent Mashinji amesema polisi wamemhoji wakitaka kujua kuhusu kauli zake za watu wasiojulikana kama anaweza kuwatambua.
“Watu wasiojulikana ambao tulikuwa tunawaongelea ni kwamba, imezoeleka kwa polisi kunapokuwa na tukio kubwa wanasema watu wasiojulikana, kwa hiyo lengo langu lilikuwa ni kuita wananchi  kurudi kwenye Polisi Jamii ili kuondokana na hili la watu wasiojulikana,” alisema Dk Mashinji.
Katibu mkuu huyo wa Chadema, leo Jumatatu ameamua kwenda kuripoti Makao Makuu ya Jeshi la Polisi jijini hapa. Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Chadema, Tumaini Makene ilisema Dk Mashinji aliambatana na wasaidizi wake kutoka makao makuu ya chama hicho.
“Katibu mkuu amewasili Makao Makuu ya Jeshi la Polisi, jijini Dar es Salaam, kuitikia wito wa Polisi uliotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto, kuwa anatakiwa kufika Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI)” alisema.
Awali, leo Jumatatu Dk Mashinji alisema  hawezi kwenda kuripoti kwa kuwa hakuambiwa siku maalumu ya kwenda.
Kamanda Muroto alimtaka Dk Mashinji afike ofisi ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai mkoani Dodoma au ofisi kama hiyo iliyopo Kituo Kikuu cha Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam ili kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo kuhusu tukio la kushambuliwa kwa risasi Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu.
“Nina taarifa za kuitwa Polisi, lakini haziko ‘specific’.  Ni wakati wowote naweza kwenda? na hawajasema nikaripoti wapi. Kwa hiyo, wakinihitaji watakuja kuniambia,” alisema Dk Mashinji leo.
Lissu alipigwa risasi na watu wasiojulikana Septemba 7 mchana alipokuwa akielekea nyumbani kwake Area D mjini Dodoma. Kwa sasa Lissu anaendelea na matibabu katika Hospitali ya Aga Khan jijini Nairobi, Kenya.

Comments

Popular posts from this blog