Zitto Kabwe: Rais Magufuli Akiniteua Nitakataa!

Rais Magufuli (kulia) akisalimiana na Zitto Kabwe, kushoto ni Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete.
KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe amesema kuwa hatokubali endapo Rais Dkt Magufuli atamteua kushika nafasi yoyote ya uongozi kwani hatakuwa na fursa ya kukijenga chama chake ili kiwe tayari kushinda uchaguzi na kushika dola.
Zitto ambaye chama anachotoka tayari kimetoa viongozi wawili ambao ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Prof. Kitila Mkumbo na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Elisha Mghwira alisema endapo atateuliwa, atamshukuru Rais na kukataa uteuzi huo.
Zitto Kabwe ambaye ni Mbunge wa Kigoma Mjini aliyasema hayo alipokuwa akifanya mahojiano na gazeti la Mwananchi wakati akijibu swali kuhusu uteuzi wa viongozi wa chama chao ambao mmoja alikuwa mshauri wa chama na mwingine alikuwa mwenyekiti wa chama hicho kichanga Tanzania.
“Sitakubali uteuzi kwa sababu jukumu langu na viongozi wengine wa ACT- Wazalendo ni kujenga chama ili kupata ushawishi  na kuungwa mkono na umma na hatimaye kushika dola,” alisema Zitto.
“Kukubali uteuzi utakaoniondoa na kuniweka kando kwenye jukumu na malengo hayo ni kufifisha matumaini ya maelfu ya wana-ACT Wazalendo,” aliongeza Zitto.
Akizungumzia sababu za chama kuridhia uteuzi wa Prof. Mkumbo, Zitto alisema kwamba hapo hali ilikuwa ni tofauti kwa sababu kabla na baada ya uteuzi wa Mkumbo, yeye ni mtumishi wa umma, hivyo uteuzi wake haukushtua.
“Mama Anna Mghwira alikuwa ni mwanasiasa kwa nafasi yake ya uenyekiti Taifa, ndio maana tulimuondoa ili kumpa fursa kutumikia serikali.”

Comments

Popular posts from this blog