Wanaomuua Jini Kabula Wajulikana!


WAKATI hali ya staa wa filamu Bongo, Miriam Jolwa ‘Jini Kabula’ ikiwa bado si shwari, watu ambao wanatajwa kuzidi kumuweka kwenye wakati mgumu na kumsukumizia kwenye kifo wamejulikana, Ijumaa linakupa habari hii ya kusikitisha.

Akizungumza na gazeti hili hivi karibuni, Jini Kabula anayedaiwa kuwa na tatizo la kuchanganyikiwa, alisema anashangaa wakati yuko kwenye matatizo hayo mazito ndipo ndugu na marafiki zake wanamtenga, hali ambayo inaweza kukatisha uhai wake.

Alisema anapitia kwenye changamoto nzito kimaisha ambapo anahitaji msaada kutoka kwa watu wake wa karibu lakini kinachomsikitisha ni kwamba, anakimbiwa na kupewa kila aina ya jina baya likiwemo la kuitwa kichaa. “Nimeteswa na kuumizwa sana, eti mimi naitwa kichaa, kweli mimi naweza kuwa kichaa, ama kweli hii dunia ni katili sana na kwa hali hii nitakufa.

“Naomba ifahamike kwamba nina matatizo makubwa sana, napitia mateso mazito, nimetengwa na watu wananikimbia, hata wale ambao tulikuwa tunasaidiana leo hii wananiona sifai, nitaishije na hali hii sasa,” alihoji Kabula huku akionekana kukataa tamaa ya maisha.

…Akionyesha makovu kwenye mwili wake.

Kutokana na maelezo yake, licha ya kwamba kweli anaonekana kutokuwa sawa kiakili, maisha ya Jini Kabula yanaweza kufikia ukingoni endapo hata marafiki na ndugu zake wataendelea kumtenga kwani ndiyo wanaotajwa kumuelekeza kwenye kifo.

Wakiongea na gazeti hili mara baada ya kutoka kwa habari ya msanii huyo kudai alipimwa Ukimwi kwa nguvu kisha kuanzishiwa dozi, baadhi ya wadau wamesema kuwa ni vyema njia sahihi zikatumika katika kumsaidia. “Unajua Kabula ni staa, yawezekana kabisa ana tatizo kubwa lakini dawa ya tatizo ni kulitatua, huenda wapo wanaohangaika kumsaidia lakini endapo ataachwa kwenye hali aliyokuwa nayo, tutampoteza.

“Leo hii Kabula anakosa pa’ kulala, kila mtu anamkimbia, sasa kama akili zake haziko sawa, apelekwe basi sehemu sahihi akapate matibabu kuliko kumuacha anatangatanga kama mtu asiye na ndugu wala marafiki,” alisema Sele Kiota wa Magomeni aliyedai kuwahi kufanya kazi na staa huyo.
…Akifanya mahojiano na GlobalTV Online.

Mwingine aliyetupia maoni yake kwenye habari iliyowekwa katika mtandao wa Global Publishers aliyejitambulisha kwa jina la Kevy, aliandika: “Walahi kwa hali hii tunamuua Kabula, maisha yake yamegeuka kuwa mabaya ghafla, anastahili kufanyiwa kitu kuokoa maisha yake.”

Hivi karibuni, Jini Kabula alitinga kwenye ofisi za gazeti hili na kueleza mazingira magumu anayopitia huku akionekana kabisa kuwa ni mgonjwa aliyekosa muelekeo wa maisha. Gazeti la Ijumaa linamuombea kwa Mungu staa huyo apone ili arejee kwenye mishemishe zake kama kawaida.
Na: BRIGHTON MASALU, DAR

Comments

Popular posts from this blog