Shamba jingine la Sumaye lachukuliwa

WAKATI machungu ya kupoteza shamba lake lenye ukubwa wa ekari 33 lililokuwa Mabwepande yakiwa hayajatuliwa, aliyekuwa Waziri Mkuu Katika serikali ya awamu ya tatu, Frederick Sumaye amepoteza shamba jingine mkoani Morogoro baada ya serikali kulichukua.
Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero imelitwaa shamba la Sumaye lenye ukubwa wa ekari 326 baada ya kupata kibali kutoka kwa Rais Magufuli kwa madai kuwa hajaliendeza licha ya kupewa notisi ya kufanya hivyo.

Shamba la Sumaye la Mabwepande lilichukuliwa Novemba mwaka jana na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi akifikia uamuzi huo baada ya mmiliki wa shamba hilo kutoliendeleza kama notisi ya siku 90 aliyopewa ilivyokuwa ikimtaka. Oktoba 28 Rais Magufuli alibatilisha umiliki wa shamba hilo namba 3,074 lililopo Mabwepande. Shamba hilo lilikuwa na hati namba 53086 na jina la umiliki lilikuwa ni Frankline Sumaye.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, Florent Kyombo jana alisema kuwa Rais Magufuli amekubali kufutwa kwa umiliki wa shamba hilo kupitia ilani ya ubatilisho ya Mei mwaka huu.

Kabla ya kutangaza uamuzi huo jana, Mkurugenzi huyo alisema kwamba Sumaye alipewa notisi ya siku 30 ya kueleza sababu za kutoendeleza shamba hilo kwa shughuli za kilimo kama lilivyosajiliwa, lakini maelezo aliyetoa yalielezwa kuwa hayakuwa na mashiko kiasi cha kuweza kubadili uamuzi huo.
Imeeleza kwa licha ya Sumaye ambaye ni Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Pwani kuendeleza sehemu ndogo ya shamba hilo lakini amekiuka Sheria ya Mipango Miji Namba 8 ya mwaka 2007 pamoja na Sheria ya Ardhi namba 4 ya 1999.

Kwa mujibu wa sheria hizo, Sumaye alitakiwa kulitumia shamba hilo kwa shughuli za kilim0 na si ufugaji.
Kyombo alisema kwamba, ndani ya miezi minne watakuwa wamemaliza taratibu za kuligawa shamba hilo kwa wananchi ili waweze kufanya shughuli za kilimo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyoanza kusambaa kwenye mitandao ya kijamii jana asubuhi ikionyesha kuandikwa na Sumaye, ilieleza tukio hilo la kunyang’anywa shamba, akisema kuwa ni kutokana na sababu za kisiasa.

“Kwangu mambo siyo mazuri, mtakumbuka baada tu ya kuingia upinzani serikali ilitishia muda mrefu kuchukua mashamba yangu bila sababu za msingi, hata wakati wa kampeni baadhi ya viongozi wa CCM walitamka hadharani kuwa huyu dawa yake ni kumnyang’anya mashamba yake. Shamba la Mabwepande ekari 33 wameagiza wiki hii halmashauri iligawe kwa wavamizi na wengineo.”
Aidha, Sumaye katika taarifa hiyo alionyesha kusikitishwa na madai kuwa shamba hilo la mvomero hajaliendeleza ambapo alisema katika shamba hilo kuna mifugo yake, mashine mbalimbali, visima vya maji pamoja na mazao.

“Jana nimepokea barua kuwa shamba la Mvomero ekari 326 limetwaliwa na Rais na sitakiwa kukanyaga hapo. Shamba hilo lina majengo, mazao, mashine mbali mbali, visima virefu vya maji, umeme na mifugo mchanganyiko zaidi ya 200. Kisingizio shamba halijaendelezwa! Shamba lenye vitu vyote hivyo halijaendelezwa?? “
Sumaye alieleza kwamba tayari alishafungua kesi katika Mahakama Kuu kwa mashamba yote na mahakama imeweka zuio la kutokuingiliwa mashamba hayo mapaka mashauri ya msingi yatakapoamuliwa lakini serikali imeamua kukaidia uamuzi huo.

Comments

Popular posts from this blog