Mahakama imeelezwa Sethi wa IPTL Amewekwa Puto Tumboni

Upande wa utetezi umeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa Mmiliki wa Kampuni ya kufua umeme ya IPTL, Harbinder Singh Sethi amewekewa ‘Puto’ tumboni kutokana na ugonjwa unaomkabili hivyo asipohudumiwa inavyotakiwa anaweza kupoteza maisha.

Mbali ya Seth, mwingine ni Mfanyabiashara James Rugemarila ambapo kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 12, yakiwemo ya kutakatisha fedha na kuisababisha Serikali hasara ya TSh 309,461,300,158.

Wakili wa utetezi, Joseph Mwakandege amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa mteja wake Seth anatakiwa apelekwe Hospital ya Taifa Muhimbili lakini hadi sasa hajapelekwa na ni dhahiri upande wa mashtaka umedharau amri mbili za Mahakama.

”Ugonjwa uliosababisha Seth atakiwe kwenda Muhimbili ni baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa ambapo tumboni kwake kumewekwa Balloon ‘Puto’ hivyo asipohudumiwa ipasavyo inaweza kusababisha kifo, naomba mshtakiwa apelekwe Muhimbili kwa sababu ni Hospitali ya juu na yenye vifaa na watalaamu wa kutosha“


Akijibu hoja hizo, Wakili wa Serikali Vitalis Peter amedai kuwa Magereza hawapangiwi wampeleke wapi mshtakiwa ambaye ni mgonjwa bali wana utaratibu, Hospitali na watalaam wao.

”Mshtakiwa alianza kupelekwa Hospital ya Magereza, kisha Hospital ya Amana ambapo alikutana na daktari mtalaam kutoka Muhimbili na aliweza kumuangalia afya yake, hivyo hoja ya kwamba hatujatekeleza amri ya Mahakama sio kweli.”

Baada ya kusema hayo, Hakimu Shahidi amesema alishatoa amri mara mbili kwamba Seth akatibiwe Muhimbili na kusisitiza akatibiwe >>>”Nasisitiza tena, mshtakiwa akatibiwe Muhimbili, sioni kama kuna sababu ya kulumbana, kesi imeahirishwa hadi September 14, 2017.”

Comments

Popular posts from this blog