Mganga aua, aondoka na kiganja cha mkono


WATU watatu wamefikishwa mahakamani akiwemo mganga wa kienyeji kwa tuhuma za mauaji ya Elizabeth Charles (45), mkazi wa kijiji cha Tambalale kata ya Nsimbo wilayani hapa.

Waliofikishwa mahakamani hapo ni Juma Idd(25), Tatu Juma (20) wote wakazi wa kijiji cha Tambalale pamoja na mganga wa kienyeji, Shida Mwanansimbila (54) mkazi wa kijiji cha Kipungulu kata ya puge wilayani Nzega.

Mwendesha mashitaka wa jeshi la polisi wilaya, Mengo Kamangala alidai mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi, Ajali Milanzi kuwa Mei 25 mwaka huu majira ya saa 5:00 usiku katika kijiji cha Tambalale Tarafa ya Nsimbo wilaya hapa, washitakiwa wote kwa pamoja walimpiga kisha kumuua na kuondoka na kiganja chake cha mkono wa kulia.

Alisema washitakiwa wote kwa pamoja walitenda kosa hilo kinyume na kifungu 196 kanuni ya adhabu sura ya 16 mapitio ya 2002 inayozuia kutenda makosa kama hayo. Hata hivyo, washitakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza shauri hilo ambapo kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 23 mwaka huu, itakapotajwa tena na washitakiwa wamepelekwa mahabusu.

Comments

Popular posts from this blog