BABU KIKONGWE WA MIAKA 80 AISHI KWA KULA UDONGO


 

Katika hali ya kushangaza na kusikitisha sana, kikongwe mmoja aitwaye Athuman Ngusa Kulaba (80) amekuwa akiishi kwa kula udongo wa nyumba anayoishi kwa sababu ya kukosa chakula cha kibinadamu.Kikongwe huyo alikutwa na Uwazi hivi karibuni nyumbani kwake, Chanika wilayani Ilala, Mkoa wa Dar es Salaam baada ya majirani kusema kwamba wamekuwa wakimshuhudia akipata mlo huo kwa karibu mwaka mmoja sasa.

Baada ya kuona hali yake inazidi kuwa mbaya, mjumbe wa eneo hilo, John Kanguya na majirani  zake walimchukuwa hadi kwenye Kituo cha Afya cha Chanika kwa ajili ya kumpima afya yake ambapo madaktari walisema tayari alipatwa na ugonjwa wa safura ambapo tumbo lake limejaa minyoo.
Uwazi lilishuhudia sehemu kubwa ya ukuta wa nyumba anayoishi kikongwe huyo ikiwa imemeguka kwa ajili ya kuchimbuliwa na kuliwa.
Majirani walilieleza Uwazi kwamba, nyumba anayoishi kikongwe huyo aliachiwa kuilinda na mtu aliyetajwa kwa jina moja la Musada karibu miaka 20 iliyopita bila kupewa huduma nyingine zikiwemo fedha.Akizungumza na Uwazi kwa lugha ya Kisukuma, kikongwe huyo alikiri kuwepo kwenye nyumba hiyo kwa miaka 20. 

Alisema awali alikuwa akipewa pesa na tajiri yake lakini baadaye utaratibu huo ukafa hivyo kwa sababu ya kukosa pesa ya kujikumu ndiyo akaamua kula vyakula vya ajabu, ukiwemo udongo wa ukuta wa nyumba hiyo.
Alisema anawashukuru majirani wa eneo hilo ambao wameweza kutambua maisha magumu anayoishi na kuamua kumpeleka hospitali na kumsaidia chakula.“Kwa sasa naomba Watanzania wenzangu wanisaidie nauli ili niweze kurudi kwetu Bukene, Tabora, maisha hapa ni magumu sana,”alisema kikongwe huyo.

Kwa Watanzania watakaoguswa na maisha magumu ya mzee huyo wanaweza kumsaidia nauli kwa kutumia namba ya simu ya Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Chanika, Mohamed Katungi 0784 295833 au 0715 295833.



Imeandikwa  na  Gazeti  la  Uwazi/gpl

Comments

Popular posts from this blog