Mwigulu Nchemba: Bado Hatuna Sheria ya Kuthibiti Shisha

DODOMA: Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba bungeni leo amesema serikali bado haina sheria ya kuthibiti matumizi ya kilevi aina ya shisha ila lipo agizo la Waziri Mkuu la kupiga marufuku biashara hiyo na kutaka agizo hilo lifuatwe na kila mtu.
Mwigulu Nchemba amesema hayo wakati akijibu swali bungeni kuhusu matumizi ya kilevi hicho cha shisha ambacho bado katika baadhi ya maeneo kimeendelea kutumika na kuleta athari kwa watumiaji.
“Ni kweli serikali baada ya kuona matumizi ya kilevi cha Shisha yanaleta athari kwa binadamu, serikali imeanza kuweka sheria za kuthibiti matumizi ya shisha, usambazaji wa shisha na uagizaji wa kilevi hicho, lakini wakati tunasubiri sheria hizo tunatambua kuwa lipo agizo la Waziri Mkuu la kupiga marufuku matumizi ya kilevi cha shisha ambalo utekelezaji wake ulianza mikoani kama Dar es Salaam, Mbeya, Iringa na mikoa mingine imeendelea kuitikia. Kwa hiyo maelekezo ya Mh. Waziri Mkuu yanafanyiwa kazi bila kupunguza hata nukta” alisema Mwigulu Nchemba
Mbali na hilo Waziri Mwigulu alisema anatambua wapo watu walipewa leseni kwa ajili ya kufanya biashara hiyo ya shisha lakini kwa kuwa serikali inajali masuala ya afya ya Watanzania ndiyo maana wanatakakuja na sheria ili kuthibiti kilevi hicho ambacho kina athari kwa watumiaji.

Comments

Popular posts from this blog