EVERTON KUCHEZA NA SIMBA AU YANGA,JULAI 13 UWANJA WA TAIFA JIJINI DAR ES SALAAM


Timu ya Everton ya England yenye wachezaji nyota akiwemo Mbelgiji, Romelu Lukaku, itazuru Tanzania kucheza mechi za kujiandaa na msimu mpya wa 2017/18, tovuti ya klabu hiyo imeandika.
Ziara hiyo ambayo itakuwa sehemu ya sherehe zao za udhamini mpya wa kampuni ya SportPesa, itaifikisha The Blues kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam unaomeza mashabiki 60,000 kucheza mechi Alhamisi ya Julai 13. Everton itakuwa timu ya kwanza ya Ligi Kuu ya England daima kucheza mechi ukanda wa Afrika Mashariki – na itamenyana na bingwa wa mashindano ya SportPesa Super Cup. Nchi mbili, Tanzania na Kenya zitakutanisha timu zao nane, nne kutoka kila upande katika michuano hiyo, kuwania nafasi ya kucheza na kikosi cha Ronald Koeman. 
Mapema mwezi huu, Everton ilitangaza udhamini mnono wa rekodi na SportPesa wa miaka mitano na baada ya hapo kampuni hiyo ikaingia Afrika Mashariki kufunga ndoa na klabu kadhaa kubwa, zikiwemo SImba na Yanga.
Michuano ya SportPesa Super Cup inatarajiwa kuanza Juni 5 hadi 11 mjini Dar es Salaam, ikishirikisha timu za Simba SC, Yanga SC, Singida United na Jang’ombe Boys za Tanzania, Gor Mahia, AFC Leopards, Nakuru All Stars na Tusker FC za Kenya.
Bingwa wa michuano hiyo itakayofanyika Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam ndiye atamenyana na Everton.

Comments

Popular posts from this blog