Ngoma, Bossou kuikosa Prisons

MSHAMBULIAJI Donald Ngoma na Vincent Bossou watakosekana katika kikosi cha Yanga kinachotarajiwa kuivaa Tanzania Prisons kutoka Mbeya katika mechi ya hatua ya ya robo ya fainali ya mashindano ya Kombe la FA itakayofanyika leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na gazeti hili jana, Kocha Msaidizi wa Yanga, Juma Mwambusi, alisema kuwa maandalizi ya mchezo huo yamekamilika na wataingia uwanjani huku wakiwaheshimu wapinzani wao kutokana na uzoefu waliokuwa nao kwenye ligi na mashindano mbalimbali.

Mwambusi alisema kuwa wamejiandaa na ushindani na changamoto kutoka kwa Prisons ambayo wachezaji wake wamekaa pamoja muda mrefu.

'Hatutawadharau Prisons, mpira hauna historia, tusubiri tuone dakika 90, ila tutamkosa Vincent ambaye ni mgonjwa aliumia jana (juzi) na leo (jana) amekwenda hospitali, Ngoma ndio hatokuwapo kabisa, aliumia tangu tulipokuwa safarii, tunasema mchezo wa kesho utakuwa mgumu zaidi, " alisema Mwambusi.

Aliongeza kuwa wamejipanga kupambana na hatimaye kushinda mechi hiyo ili waweze kusonga mbele na hatimaye kupata nafasi ya kushiriki mashindano ya Kombe la Shirikisho au Ligi ya Mabingwa Afrika endapo watatwaa ubingwa wa Ligi Kuu.

Naye Kocha Mkuu wa Prisons, Abdallah Mohammed, alisema kuwa wataingia katika mechi ya kesho wakiwa makini ili kuwadhibiti wachezaji wa Yanga ili wasipate nafasi za kufunga.

"Ni mchezo mgumu, hatuwaogopi kwa sababu sisi pia tuna kikosi kizuri, tunaamini tutapata matokeo mazuri na kusonga mbele," alisema kocha huyo.

Mshindi kati ya Yanga na Prisons ataungana na Simba, Azam FC na Mbao FC ambazo zimeshatinga hatua ya nusu fainali ya Kombe la FA, michuano hii ndiyo inatoa mwakilishi wa mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika mwakani.

Wakati huo huo, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas, alisema droo ya mechi za nusu fainali itafanyika kesho asubuhi.

Comments

Popular posts from this blog