Aliyeua mwanawe kwa nyundo atakiwa kupimwa akili

JAJI wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Joaquine De-Mello ameamuru mtuhumiwa wa mauaji ya mwanawe kwa kutumia nyundo na ambaye ni mchinja nguruwe, Ezekiel Magige akapimwe akili Dodoma.
Magige, ambaye ni mkazi wa mji mdogo wa Sirari alifikishwa mahakamani jana kwa tuhuma za kumuua mtoto wake kwa kumpiga kwa nyundo kichwani na ubongo kusambaa.
Mahakama Kuu ipo katika vikao vyake vya kikanda Tarime kwa wiki mbili na Jaji De-Mello anasaidiwa na Jaji Rose Ebrahim. Kesi zaidi ya 40 ama zitatajwa au kusikilizwa, zikihusisha makosa ya mauaji, madawa ya kulevya na ujambazi wa kutumia silaha.
Wakili wa Serikali, Harry Mbogoro alidai kuwa Desemba 28, 2014 na akiwa nyumbani kwake Sirari, mtuhumiwa Magige alimpiga kwa nyundo kichwani mwanawe Julias Michael na kusababisha kifo chake papo hapo.
Jaji De-Mello alisema "ninaagiza mtuhumiwa huyu Ezekeil Magige apelekwe Isanga Dodoma kupimwa akili kabla ya kusikilizwa kwa kesi yake kwani tukio hili sio la kawaida.
" "Mtu mwenye akili timamu (anaweza) kumuua mtoto wake kwa kumpiga kwa nyundo kichwani mtoto wake hadi ubongo kusambaa?" Katika kesi nyingine, mfanyabiashara Tumaini Wankyo (28) alihukumiwa kwenda jela mwaka mmoja baada ya kupatikana na hatia ya kumuua bila kukusudia.
Wankyo alikuwa ameshitakiwa kwa kumuua bila kukusudia askari Jeshi la Wananchi, Rojar Elias kwa kumpiga risasi, wakati wakigombea mwanamke hotelini.
Katika kikao cha Mahakama Kuu kwenye Mahakama ya Wilaya Tarime, Wakili Mbogoro alidai kuwa mauaji hayo yaliyokea Agosti 17, 2015 saa 7 usiku katika Hotel ya NK iliyopo mjini Tarime.
Ilidaiwa kuwa mtuhumiwa akiwa na mpenzi wake wa kike wakila chakula na vinywaji, alifika askari Elias akiwa na wenzake wawili na kutaka kumchukua mwanamke huyo kwa nguvu.
Ilielezwa kuwa katika kutekeleza azma hiyo, Elias alimshambulia Wankyo kwa kumpiga ngwara na kumwangusha chini akiwa na bastola iliyokuwa na risasi kwenye chemba.
Wakili wa Serikali Mbogoro alidai katika purukushani hiyo risasi moja ilichomoka kutoka kwenye bastola ya Wankyo anayomiliki kihalali na kumjeruhi askari huyo ambaye alifariki akipatiwa matibabu Hospitali ya Bugando, Mwanza. Jaji De-Mello alimuhukumu kwenda jela mwaka mmoja.

Comments

Popular posts from this blog