Wananchi wa Cuba Watoa Heshima za Mwisho Kwa Mwili wa Rais Fidel Castro



fidel-castro-1
HAVANA, CUBA: Maelfu ya raia wa Cuba wanatoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi mwanamapinduzi Fidel Castro, aliyeaga dunia Ijumaa iliyopita akiwa na umri wa miaka 90.
Ikiwa ni siku ya kwanza ya kipindi cha siku tisa za maombelezi rasmi ya kifo chake, misafara mirefu imeshuhudiwa katika uwanja wa Revolution Square katika Mji Mkuu Havana, sehemu ambayo waombolezaji wameweka picha ya kiongozi huyo akiwa ameshika bunduki.
fidel-castro-1
Siku za maombolezi zitakamilika baada ya majivu ya mwili wake kuzikwa siku ya Jumapili. Majivu ya Castro yalitazamiwa kuwasilishwa kwa umma katika uwanja wa Revolution Square lakini yamewekwa katika sehemu tofauti.
‘Roho ya Cuba’
Wananchi wengi wa Cuba walikuwa katika milolongo hata kabla ya alfajiri kuwadia ili kuhakikisha wako miongoni mwa watu wa kwanza kutoa heshima zao.
fidel-castro-3
Tania Jimenez, mwenye umri wa miaka 53, mwanahisabati, ameliambia shirika la habari la AP kwamba Fidel ni kila kitu kwao, na ni kiungo muhimu kwa nchi hiyo aliyojitolea siku zote maishani mwake.
Castro aliingia madarakani mwaka 1959, na kuongoza mapinduzi ya Kikomunisti. Wanaomuunga mkono walisema ameirejesha Cuba kwa watu wake na wakamsifu kwa mipango ya kijamii aliyoifanya kama vile huduma za afya na elimu.
Lakini wakosoaji wamemtaja kama, dikteta, aliyeiongoza serikali ambayo haikuhusiana vyema na upinzani na kwamba hakuheshimu haki za kibinadamu.
fidel-castro-2
Mtu mwenye ushawishi
Wananchi wamekuwa wakipanga misafara mirefu eneo lenye picha kubwa ya urefu wa ghorofa tisa iliyotungikwa kwenye ukuta wa jumba, huku wengi wao wakibeba picha za kiongozi huyo.


Kwa wakati mmoja mizinga 21 ilifyatuliwa kuadhimisha mwanzo wa maombolezii rasmi mjini Havana na kusini mashariki mwa mji wa Santiago de Cuba, kutoka sehemu ambayo Castro alizindua chama cha mapinduzi mnamo mwaka 1959.
fidel-castro-2
Hali katika mji huo ni tofauti ikilinganishwa na wakati wa kifo cha kiongozi huyo kilipotangazwa. Sherehe na michezo yote iliahirishwa, huku raia wengi wa Cuba wakikusanyika kuzungumzia habari lakini walisalia kimya, mwandishi wa BBC wa Cuba alisema.
Maombolezo yakindelea, maelfu ya raia wa Cuba wanatarajiwa kuhudhuria sherehe ya makumbusho siku ya Jumatatu na Jumanne mjini Havana.
fidel-castro‘Saini ya kiapo’
Viongozi wa cuba wamesema ”Waombolezaji wataweka saini za kiapo kuahidi kutekeleza uzalendo na pia kutii kanuni ya ujamaa iliyodhihirika na kiongozi wao wa kihistoria.”


Revolution Square ndio itakuwa sehemu ambayo ibada ya misa itakapofanyika ambayo itahudhuriwa na viongozi wa kimataifa Jumanne jioni.
Rais wa Bolivia Evo Morales na Rais wa Ecuador Rafael Correa ambao ni marafiki wa karibu wa Cuba, wamethibitisha kuhudhuria huku Korea Kaskazini ikisema itatuma ujumbe hadi kisiwa cha Caribbean.
Rais wa Urusi Vladimir Putin aliyempongeza Fidel Castro kama ”rafiki wa dhati na mwaminifu kwa Urusi,” hatahudhuria.
Rais mteule wa Marekani Donald Trump, aliyemtaja Castro kama”dikteta katili” hatahuduria pia.
Bw Trump alitoa tahadhari siku ya Jumatatu kwamba huenda akafuta uhusiano ambao umekuwa ukiimarika kati ya Cuba na Marekani chini ya uongozi wa Barrack Obama. Amesema serikali ya Cuba inastahili kufanya hatua zaidi chini ya maafikiano yake na Marekani.
Siku ya Jumatatu, safari ya kuzungusha majivu ya Bw Castro itaanza Santiago de Cuba na inatarajiwa kuwa safari ya kilomita 1,000.
Majivu yake yatazikwa siku ya Jumapili katika makaburi ya mji wa Santa Ifigenia, sehemu ambayo kiongozi Jose Marti alizikwa.

Comments

Popular posts from this blog