Yanga yamuacha Kessy

Kessy
Mchezaji wa Yanga, Hassan Kessy.
Wilbert Molandi,Dar es Salaam
MSAFARA wa wachezaji 21 wa Yanga, asubuhi ya kesho Jumamosi utaondoka kuelekea nchini Ghana kwa ajili ya kukipiga na Medeama ya nchini humo huku wakiwaacha mabeki wao, Hassan Kessy na Mtogo, Vincent Bossou.
Yanga itarudiana na Medeama katika mechi ya Kombe la Shirikisho Afrika baada kutoka sare ya kufungana bao 1-1 mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Julai 16, mwaka huu.
Chini ya Kocha Mholanzi, Hans van Der Pluijm, Yanga inatakiwa kushinda kwenye mchezo huo ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kufuzu kucheza Nusu Fainali ya michuano hiyo, kinyume na hapo hali ya mambo inaweza kuwa mbaya na yawezekana wakawa wamefuta ndoto za kusonga mbele.
Hassan-‘-Kessy’-Ramadhani2
Meneja wa Yanga, Hafidh Saleh, amesema msafara wao unatarajiwa kuwa na watu 30, kati ya hao, wachezaji ni 21 na viongozi tisa.
Amesema msafara huo unatarajiwa kuondoka saa moja asubuhi kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere (JNIA) wa jijini Dar kwa Shirika la Ndege la Kenya Airways (KQ).
Kuhusu Kessy, meneja huyo amesema amebaki kwa kuwa hakuna mipango ya kumtumia kwa kuwa bado suala lake la usajili ni kikwazo.
Kuhusu Bossou hatakwenda kwa kuwa anatumikia adhabu ya kadi mbili za njano zitakazomkosesha mechi hiyo. Kiungo wa timu hiyo, Deus Kaseke naye hatakwenda kwa kuwa Pluijm ameshauri abaki kwa ajili ya kupumzika, licha ya kupona majeraha ya mwili aliyoyapata kwenye ajali ya pikipiki, pia Geofrey Mwashiuya naye atabaki kwa kuwa ana majeraha ya goti.
“Kessy bado hajathibitishwa kuichezea Yanga kutokana na lile sakata lake na Simba,” alisema meneja huyo.
Akizungumzia suala hilo la kuachwa, Kessy alisema: “Sina jinsi, ndiyo hivyo imeshatokea, nipo tu kambini kwa sasa, nasubiri wakiondoka mimi itabidi nirudi nyumbani kuwasubiri wenzangu, lakini itabidi nilisimamie mimi mwenyewe wakati wenzangu watakapokuwa Ghana. Inaniuma sana na ninasikitishwa na hali ya mambo inavyoendelea.”
Wachezaji watakaosafiri na timu ni Deogratius Munish ‘Dida’, Ally Mustapha ‘Barthez’, Beno Kakolanya, Juma Abdul, Haji Mwinyi, Oscar Joshua, Mbuyu Twite, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani, Pato Ngonyani.
Wengine ni Said Juma ‘Makapu’, Andrew Vincent ‘Dante’, Thabani Kamusoko, Haruna Niyonzima, Simon Msuva, Juma Mahadhi, Obrey Chirwa, Malimi Busungu, Amissi Tambwe, Donald Ngoma na Anthony Matheo.

Comments

Popular posts from this blog