Wabongo wafungukia simu feki kuzimwa

Simu fekiStori:  Gladness Mallya, Risasi Jumamosi
DAR ES SALAAM: Baada ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ‘TCRA’ kutangaza kuzima simu feki usiku wa Juni 16, mwaka huu, wananchi mbalimbali wa Jiji la Dar, wamefunguka ya moyoni:
BARIKI GASTON (MWENGE)
“Kuzimwa simu feki kumeniumiza sana na siyo mimi tu wapo wengi hasa wenye hali ya chini japokuwa zina madhara wangetuachia kwa muda mrefu kidogo ili tujipange kwanza.”
HIDAYA SAID (MWANANYAMALA)
“Serikali ilivyofanya siyo vizuri kwa sababu hali ya maisha ni ngumu, nafanya mama ntilie hapa sina uwezo wa kununua simu orijino, wangetuangalia sisi watu wa vipato vya chini wasingezima ila wangezuia zile zinazoingia nchini lakini hizi tunazomiliki tubaki nazo.”
JOSEPH VENANCE (MWENGE)
“Suala la simu feki kuzima limetuchanganya sana maana tulishazoea kununua kwa bei rahisi lakini sasa haya ni majanga kwa sababu mpaka upate hela ya kununua simu orijino ni kazi sana lakini inabidi tukubaliane tu hali halisi maana zina madhara pia Watanzania tujifunze kutumia vitu orijino ili kuipatia kodi nchi yetu.”
Ramadhan Omari ‘Babu Kaju’ (MWENGE)
“Kiukweli uamuzi wa serikali wa kuzima simu feki siyo sawa kabisa kwani hawajaangalia uwezo wa mwananchi kwani kuna watu wanauza maparachichi je, watamudu vipi kununua simu ambazo siyo feki? Pia muda waliotoa wa miezi mitatu ni mdogo sana walitakiwa watoe muda hata mpaka Januari mwakani ili watu wajipange maana imeniathiri sana hata mimi.
“Kwa nini wasingewabana wale wanaoingiza simu hizi feki nchini, mbona ushuru wao wanachukua? Viongozi wanatakiwa kuwa makini sana katika maamuzi yao maana siku hizi  wanaamua tu, lilikuja suala la ving’amuzi ndiyo vile watu kibao wakatupa TV zao maana hawana uwezo huo wa kununua hata kama ndiyo kwenda kidijitali siyo kwa staili hii jamani.”
PIUS NGONYANI ‘KADODA’ (MWENGE)
“Naona sawa tu serikali ilivyofanya kwa sababu vitu feki siyo vizuri pia inawezekana kuna kitu serikali inakosa kama kodi lakini kwa simu orijino kodi itapatikana na imejua madhara ya simu feki japokuwa wamechelewa sana kwani Watanzania wameshatumia kwa muda mrefu sana simu hizo wao walikuwa wapi.

Comments

Popular posts from this blog