SERIKALI KUANZISHA BENKI YA MAENDELEO YA VIWANDA NCHINI.

Na Lilian Lundo-MAELEZO.
Serikali ya awamu ta Tano imedhamiria kuifanya sekta ya Viwanda nchini kuchangia pato la taifa kwa asilimia 40 ifikapo mwaka 2020 kutoka asilimia 7.3 ya sasa.
Hayo yamesemwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli wakati wa hafla ya utoaji tuzo za Rais kwa wazalishaji Bora wa Viwandani kwa mwaka 2015 leo Jijini Dar es Salaam.
Rais Magufuli amesema kuwa jambo hilo linawezekana hasa kwa kuzingatia nchi yetu ina rasilimali zinazohitajika katika kujenga uchumi wa viwanda.“Nafahamu kwamba tunakila aina ya rasilimali inayowezesha uwepo wa viwanda hapa nchini ikiwemo umeme wa kutosha pamoja na malighafi zake na kwa maana hiyo serikali ya awamu ya tano imepanga kuifanya sekta ya viwanda kuchangia pato la taifa kwa asilimia 40 ifikapo mwaka 2020 kutoka 7.3 ya sasa”. Alisema Rais Magufuli.
Aidha Dkt. Magufuli aliwatoa wasiwasi wadau hao kuhusu uwepo wa soko la uhakika kwa bidhaa zitakazozalishwa kwani Tanzania imezungukwa na nchi zenye uhitaji wa bidhaa mbalimbali na pia ni Mwanachama wa jumuiya mbalimbali ndani na nje ya Afrika.
Naye Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage aliwataka wamiliki wa Viwanda Nchini kuunganisha nguvu katika uanzishaji na uendelezaji wa viwanda nchini ili kuongeza upatikanaji wa bidhaa nchini hali itakayopelekea kukuza uchumi wa nchi na kuongeza ajira kwa watanzania.

Comments

Popular posts from this blog