Mdosi mbaroni kwa ujambazi Moshi

Wilbrod-MutafungwaKamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, ACP Wilbroard Mtafungwa.
Issa Mnally na Richard Bukos, UWAZI
DAR ES SALAAM: Watu watatu akiwemo mmoja mwenye asili ya Kiasia ‘Mdosi,’ wametiwa mbaroni na polisi Moshi mkoani Kilimanjaro kwa tuhuma za ujambazi, Uwazi limeezwa.
Akizungumza na waandishi wetu kwa njia ya simu mwishoni mwa wiki iliyopita, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, ACP Wilbroard Mtafungwa alisema kuwa watuhumiwa hao wanashikiliwa na jeshi hilo baada ya kukamatwa kutokana na ushirikiano wa polisi na raia wema.
Akielezea jinsi polisi walivyowanasa watuhumiwa hao, Kamanda Mtafungwa alisema kuwa walimkamata kwanza mmoja Fredil Guston maarufu kwa jina la Chedieli ambaye ni mkazi wa Majengo, Moshi.
Aidha, alisema Chedieli aliwataja wenzake ambao ni Frank Nkya maarufu kwa jina la Chabufa na Frank Mbesanyo Domani ‘Ausho’ mkazi wa Pasua na walipopekuliwa walikutwa na vitu kadhaa vya wizi.
“Sasa hawa wakamtaja bosi wao ambaye ni kiongozi wao mkuu wa ujambazi, Mhindi aitwaye Multazi Mohammed (52) maarufu kwa jina la Bisuza Tazani, mkazi wa Majengo Mwembeni, Moshi.
“Huyu Mhindi ndiye mtunzaji wa silaha wanazotumia kufanyia ujambazi kwani baada ya kupekuliwa alikutwa na vitu kadhaa vya wizi na alipohojiwa alitupeleka shambani ambako anaficha silaha.
“Huko shambani alikuwa ameficha kwenye mahindi shotigani aina ya Greener yenye namba 43769 ikiwa imefungwa katika mfuko wa nailoni ikiwa imekatwa mtutu na kitako,” alisema Mtafungwa.
Aliongeza kuwa uchunguzi wao ulionesha kuwa silaha hiyo iliibwa kwa Gerard Mosha mkazi wa Rosho Kilemi, Wilaya ya Moshi Vijijini Machi, 2014 na siku ya tukio hilo Mosha alijeruhiwa vibaya kwa kukatwa panga kichwani, kupigwa na nondo na kuibiwa vitu kadhaa dukani kwake.
“Tutawafikisha mahakamani wakati wowote tukikamilisha upelelezi,” alisema.

Comments

Popular posts from this blog