Kesi ya Bosi wa TRA na Wenzake Yarudishwa Tena Mahakama Kuu

                
MISS 3
Mahakama ya Rufani Tanzania, imeamuru jalada la kesi inayomkabili Kamishna Mkuu wa zamani wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya na wenzake kurudishwa Mahakama Kuu kwa ajili ya kusikilizwa rufani ya Jamhuri.
Pia, imeagiza jalada hilo lipangiwe kusikilizwa kwa jaji mwingine dhidi ya rufaa ya kupinga kuondolewa shtaka la utakatishaji fedha katika kesi ya kujipatia Dola za Marekani milioni 6.
Hukumu hiyo ilisomwa jana na Msajili wa Mahakakama ya Rufani, Zahra Maruma baada ya kusikilizwa na jopo la majaji watatu, likiongozwa na Mwenyekiti Salum Masati akisaidiana na Kipenka Musa na Augustine Mwarija.
Msajili Maruma alisema mahakama hiyo imeona kwamba Jaji Mfawidhi Moses Mzuna alikosea kukubali pingamizi la utetezi na kutupilia mbali kusikiliza rufani ya kupinga uamuzi uliotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wa kuliondoa shtaka la kutakatisha fedha dhidi ya Kitilya na wenzake.
“Mahakama hii imebatilisha uamuzi uliotolewa na Jaji Mzuna na kwamba imeamuru jalada lirudishwe Mahakama Kuu kwa ajili ya kupangiwa jaji mwingine wa kusikiliza rufani ya upande wa Jamhuri kuhusu kuondolewa kwa shtaka hilo” alisema Msajili na kuongeza.
 
“Kwa kuondolewa shtaka hilo Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP) hakuwa na namna ya kurudi Mahakama ya Kisutu kuomba kufanya mabadiliko ya hati ya mashtaka kwa sababu kila shtaka linajitegemea na kwamba shtaka la kutakatisha fedha lilishaondolewa na kumalizika katika hati hiyo ya mashtaka dhidi ya washtakiwa” alisema Msajili Maruma wakati akisoma hukumu hiyo.
Akifafanua zaidi alisema Mahakama ya Rufani imebatilisha uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu na kuamuru kusikilizwa rufani ya DPP kama ilivokuwa imekatwa.
Mapema Mei 31, mwaka huu upande wa Jamhuri ukiongozwa na DPP, Biswalo Mganga, Naibu DPP, Osward Tibabyekomya, Mawakili wa Serikali Waandamizi, Shadrack Kimaro na Awamu Mbagwa uliomba mahakama hiyo kuangalia uhalali wa kuondolewa shtaka la kutakatisha fedha pamoja na uamuzi wa Jaji Mzuna kutupilia mbali rufani yao.
“Watukufu Majaji ni rai yetu upande wa Jamhuri, tunaomba  mahakama hii iangalie upya na kuiamuru Mahakama Kuu kusikiliza rufaa ya kuliondoa shtaka la kutakatisha fedha …”alidai DPP Mganga.
Akiwasilisha hoja za rufaa hiyo mahakamani hapo, Tibabyekomya alidai kuwa malalamiko yao ni kwamba Jaji Mfawidhi, Mosses Mzuna alikosea kukataa kusikiliza rufaa ya kuondolewa kwa shtaka hilo na mahakama ya chini.
Alidai kuwa kinachashtakiwa katika shtaka ni kosa ambalo limekamilika na kwamba linasisimama kwa kujitegemea.
 
“Watukufu majaji kitendo cha kufuta kabisa shtaka la nane la kutakatisha fedha dhidi ya washtakiwa kulihitimisha shtaka hilo kama lilivyokua limeshtakiwa  kwa kuwa lilikuwa linajitegema”alidai na kuongeza kuwa.
“Jaji Mzuna alikataa kwamba mahakama yake haina uwezo wa kuruhusu kufanya mabadiliko ya hati ya mashtaka na kwamba uamuzi huo ulionyesha haiwezekani kufanyika mabadiliko amri ambayo inahitimisha shtaka la nane” alidai msaidizi huyo wa DPP.
Mawakili wa utetezi wakijibu hoja za Jamhuri kwa nyakati tofauti; Wakili Majura Magafu alidai kuwa rufaa hiyo haina mashiko ya kisheria na kwamba ilifunguliwa mapema kinyume cha sheria mahakama hiyo itupilie mbali.
“Hakimu Mchauru hakukosea kama inavyodaiwa na Jamhuri kwa sababu alitoa nafasi kwamba wakati utakapofika kisheria wataruhusiwa kufanya mabadiliko… “alidai Magafu.
Dk. Ringo Tenga alidai kuwa baada ya kuondolewa shtaka hilo, upande wa Jamhuri haukuwasilisha maombi ya kufanya mabadiliko ya hati ya mashtaka.
Alex Mgongolwa alidai kuwa hoja zao za utetezi kwamba rufaa hiyo haina sababu za kutosholeza kisheria imefunguliwa kinyume cha sheria mahakama ifutilie mbali.
Mbali na Kitilya, washtakiwa wengine ni, aliyekuwa Miss Tanzania mwaka 1996, Shose Sinare na mwanasheria wa benki ya Stanbic Tanzania, Sioi Solomon.

Comments

Popular posts from this blog