Mkuu wa Mkoa wa Arusha apiga marufuku uuzwaji kinywaji cha KIROBA.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Felix Ntibenda amepiga marufuku uuzwaji wa kilevi aina ya kiroba katika mkoa huo.Alisema uamuzi huo unatokana na vijana ambao ni nguvu kazi ya taifa kushindwa kufanya kazi na kulewa wakati wa kazi.Aidha mkuu huyo wa mkoa alisema anafanyia kazi sakata la mkazi wa Kata ya Ngarenaro anayedaiwa kujihusisha na uuzaji na uingizaji wa dawa za kulevya ambaye baada ya kukamatwa na polisi aliachiwa katika mazingira ya kutatanisha.
Ntibenda alisema hayo jana Arusha wakati akizungumza na watendaji wa serikali za mitaa 154, maofisa watendaji kata 25 pamoja na wenyeviti wa serikali za mitaa.
Alisema suala la kilevi aina ya kiroba ni kero kwa vijana kufanya kazi wakiwa wamelewa au kuwa navyo mifukoni hasa madereva wa pikipiki, daladala na wapiga debe.
Alisema kutokana na vijana kunywa kinywaji hicho nyakati za kazi, amepiga marufuku uuzwaji wa kilevi hicho, atakayekiuka agizo hilo hatua za kisheria zitachukuliwa.
“Sitaki kuona viroba vikiuzwa katika Mkoa wa Arusha na atakayekiuka nitamchukulia hatua za kisheria, lakini huyu anayeuza dawa za kulevya halafu polisi wanamwachia na wananchi hawajui kwanini anaachiwa huku akiendelea kuuza dawa, sasa nasema mwisho wake umefika, nitafuatilia kwa makini suala hili.”

Baadhi ya wenyeviti wa serikali za mitaa walihoji sababu za kutokuwa na ofisi za kufanyia kazi badala yake wanalazimika kutumia nyumba zao au kukodisha ofisi ili kufanya kazi za jamii lakini pia hawana posho za vikao.

Wenyeviti hao akiwemo Amani Mwakalinga wa mtaa wa Darajani na Hilary Mkonyi wa mtaa wa Ngarenaro, walisema awali Mkurugenzi wa Jiji, Juma Idd aliahidi kuwajengea ofisi lakini hadi sasa hakuna utekelezaji.

Comments

Popular posts from this blog