RAIS MAGUFULI AWATAKA WATANZANIA KUJIFUNZA KUTOKA KWA VIETNAM

Na. Lilian Lundo - Maelezo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amewataka watanzania kujifunza kutoka kwa Vietnam namna ambavyo wameweza kupambana na umaskini kwa muda mfupi.
Mhe. Rais aliyasema hayo leo Ikulu katika ziara ya Rais wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam Mhe. Truong Tan Sang baada ya kusaini mkataba wa kukuza uhusiano baina ya Tanzania na Vietnam.
“Tanzania tunatakiwa tujifunze mambo mengi kutoka kwa wenzetu Vietnam ambao walipata uhuru mwaka 1945 wakaingia kwenye mapigano mpaka mwaka 1976. Wakati huo pato la muvietnam mmoja lilikuwa dola 100 lakini leo ni dola 2000 na wamepunguza umaskini kwa asilimia 50 kuifanya nchi hiyo kuwa ya kipato cha kati,” alisema Mhe. Rais
Mhe. Rais Magufuli aliongezea kuwa, mwaka 1976 Vietnam ilichukua mbegu ya korosho kutoka Tanzania na kwenda kulima kwao, zao hilo limekuwa likifanya vizuri kwa nchi yao na wanaongoza kwa kulima korosho Duniani. Kwa upande wa Tanzania zao hilo limekuwa likitelemka chini kila mwaka.

Vilevile, Mhe Rais alisema kuwa Vietnam ni nchi inayoongoza kwa uzalishaji wa samaki lakini Tanzania ambayo ina maziwa 21 pamoja na mito na bahari kila mahali haijaweza kuifikia Vietnam kwa uzalishaji wa samaki hivyo lazima watanzania tujifunze na tusiogope kujifunza ili Tanzania itoke mahali iliko.

Aidha Mhe. Rais alisema ziara ya Vietnam imekuja wakati muafaka wa kujenga mahusiano mazuri kwa watanzania na nchi ya Vietnam lakini hasa katika uchumi ili Tanzania iweze kufanikiwa namna ambavyo wao wamefanikiwa. 

Kwa upande wake, Mhe. Rais Truong alimshukuru Rais Magufuli na watanzania kwa mapokezi mazuri na ameahidi kuimarisha mahusiano ya nchi hizi mbili hasa katika sekta ya kilimo, biashara, mawasiliano pamoja na uwekezaji.

Mhe. Rais Truong Tan Sang ni Rais wa kwanza wa nchi ya Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam kufanya ziara nchini Tanzania. Rais huyo ameambatana na mawaziri wanne pamoja na wafanyabiashara wapatao 30. 
Mahusiano ya Tanzania na Vietnam yalijengwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Kiongozi wa Vietnam, Ho Chi Minh kuanzia mwaka 1960 na kupelekea kuanzishwa rasmi kwa mahusiano ya kidiplomasia mwaka 1965.

Comments

Popular posts from this blog