MAMA: Miezi 11 Mwanangu Anaishi Kwa Mateso Bila Upasuaji!


Mtoto Asmina Abdallah.
Makongoro Oging’ na Haruni Sanchawa
Mtoto Asmina Abdallah mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi minne, mkazi wa Kijiji cha Mgambo, Unguja, Zanzibar anaishi kwa mateso bila kufanyiwa upasuaji kwa madai ya kutokamilika kwa vipimo kufuatia upungufu wa mashine katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Mtoto Asmina Abdallah akiwa na mama yake, Amina Maburuki Amani.Maisha ya mtoto huyo kwa sasa yapo hatarini kutokana na uvimbe uliopo machoni kuongezeka na haujapatiwa ufumbuzi wa matibabu kwa miezi 11 huku ukienda sambamba na maumivu makali. 
Akizungumza na waandishi wa habari hii wiki iliyopita katika wodi ya watoto ya Makuti A Muhimbili, mama mzazi wa mtoto huyo, Amina Maburuki Amani alisema kwamba hali ya mtoto wake inazidi kuwa mbaya na anaelekea kukata tamaa. 

Akifafanua zaidi mama huyo alikuwa na haya ya kusema: 
“Hali ya mtoto wangu imekuwa ikibadilika kila kukicha huku akilia kutokana na maumivu makali, nimechoka safari ya kila mara ya kuja Muhimbili kwa nauli ya kuombaomba kwa wasamaria mema. 
“Maisha yangu yako duni, najua ipo siku nitashindwa kuja, sina kazi na wala sijui mume wangu aliko. 

“Tangu uvimbe huu umuanze mwanangu ukiwa kama upele Januari mwaka huu, umekuwa ukiongezeka, nilifika Muhimbili kwa mara ya kwanza Januari mwanzoni lakini Aprili mwaka huu nikarudishwa nyumbani kutokana na ukosefu wa mashine ya CT Scan. 
“Nililazimika kuja tena Muhimbili Juni nilikaa kidogo nikaambiwa kipimo hicho kiko katika hospitali binafsi hivyo zinahitajika fedha, nikalazimika kwenda nyumbani kutafuta bila mafanikio. 

“Hali ya mtoto ilizidi kuwa mbaya nikaomba nauli kwa majirani nikamleta hapa Muhimbili, Mama Salma Kikwete yaani mke wa rais mstaafu wa awamu ya nne alinisaidia shilingi laki nne na nusu na baadhi ya wasamaria wema walinichangia baada ya kuona habari yangu katika gazeti hili. 
“Nikafanyiwa kipimo cha CT Scan katika Hospitali ya Besta lakini hata hivyo hakupata matibabu kutokana na kutokamilika kwa vipimo vingine. 

“Niliambiwa na uongozi wa Muhimbili kuwa angeweza kwenda India lakini sioni matarajio, Agosti 20 nikarudishwa nyumbani, baadaye hali ya mtoto ikazidi kuwa mbaya akawa anazimia. 
“Nililazimika kumleta tena hapa Muhimbili Oktoba 7, amepimwa damu na sasa nasubiri matokeo pia nijue nini kitaendelea.”
Kwa yeyote aliyeguswa na kilio cha mama huyu awasilianenaye kwa namba yake ambayo ni 0658 323590.

Comments

Popular posts from this blog