WASIRA ,BULAYA WALALAMIKIA HUJUMA


Bunda. Wagombea ubunge Jimbo la Bunda Mjini, Stephen Wasira (CCM) na Ester Bulaya (Chadema), wameomba vyombo vya ulinzi kusimamia amani kipindi hiki cha kampeni inayoonekana kuvurugwa na baadhi ya wafuasi wa vyama hivyo.
Kauli hizo zilitolewa na wagombea hao kwa nyakati tofauti kwenye mikutano yao na waandishi wa habari juzi. Walidai baadhi ya wafuasi hutishiana maisha na wengine kupigana hadi kujeruhiana.
Juzi saa tatu asubuhi, Bulaya aliitisha mkutano na waandishi wa habari akilalamikia wafuasi wa chama hicho kupigwa hadi kujeruhiwa, huku mikutano yake ya kampeni ikifanyiwa fujo na watu wanaodaiwa ni wafuasi wa CCM na vyombo vya dola havikuchukua hatua.
Wasira aliomba vyombo vya ulinzi na usalama hususan polisi, kutamka wazi kama wamezidiwa na kazi, ili aombe kwa mamlaka za juu kuongeza polisi watakaosaidia kuimarisha amani na utulivu kwenye mikutano yake ya kampeni.
Wasira alisema wajibu wa polisi ni kulinda usalama wa raia na mali zao, lakini hawafanyi hivyo. Watu wanaishi kwa hofu kutokana na vitisho vya wafuasi wa vyama vya siasa.
“Wanajeruhi watu kwa mapanga, wanaponda magari mawe, polisi lazima wachukue hatua,” alisema Wasira.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Phillip Kalangi aliahidi kufuatilia ili hatua zichukuliwe ikiwezekana hata kuwakamata wahusika na kuwafikisha mahakamani.

Comments

Popular posts from this blog