WAJAWAZITO 1,500 WAKUTWA NA VVU

MIMBAAAA_dc0f3.jpg
JUMLA ya wanawake wajawazito 1,576 kati ya 42,712 waliopima Virusi Vya Ukimwi (VVU) mwaka jana katika vituo mbalimbali vinavyotoa huduma za afya mkoani Pwani walipatikana na maambukizi ya ugonjwa huo.
Takwimu hizo zilitolewa mjini Kibaha juzi na Mratibu wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (Tacaids) Mkoa wa Pwani, Hafidh Ameir, wakati wa ziara ya Kamati ya Bunge ya masuala ya ukimwi na dawa za kulevya ilipotembelea mkoani hapa.
Ameir alisema pamoja na takwimu hizo, lakini kwa sasa maambukizi ya VVU mkoa huo yamepungua kutoka asilimia 6.7 mwaka 2008 hadi kufikia asilimia 5.9 kwa mwaka 2012 kutokana na jitihada mbalimbali.

Alisema kwa sasa mkoa una vituo vya tiba 263 na kati ya hivyo vituo 214 sawa na asilimia 81 vinatoa huduma ya upimaji wa hiari na ushawishi wa VVU na vituo 52 vinatoa huduma ya dawa za kufubaza makali ya VVU kwa watu wanaoishi na VVU ambavyo ni asilimia 24 ya vituo 214.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Lediana Mng'ong'o, alitoa wito kwa halmashauri kushirikisha kikamilifu wadau ikiwa ni pamoja na kuweka wazi taarifa zao za vikao.
Mng'ong'o ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu, alisikitishwa na kitendo cha kutokuwepo kwa viongozi wa kisiasa kwenye kikao cha kamati hiyo na wataalamu wa halmashauri, hivyo kutoa wito wa kushirikishwa kwa viongozi hao ili wajue taarifa muhimu za wananchi wao.
Kamati hiyo ya Bunge iko kwenye ziara ya siku mbili mkoani Pwani katika Wilaya ya Kibaha Vijijini na Bagamoyo.
CHANZO:TANZANIA DAIMA

Comments

Popular posts from this blog