MCHUNGAJI ADAI KUWAUA SHARO, KANUMBA

Mwanaume aliyetambulishwa kwa jina la Mchungaji Mayanga amewashangaza waumini baada ya kudai kanisani kuwa yeye ndiye aliyewaua mastaa wawili Bongo, Hussein Ramadhan Mkiety ‘Sharo Milionea’ na Steven Kanumba ‘The Great’.
Mchungaji Mayanga (mwenye kipaza sauti) akitoa ushuhuda.
Tukio hilo lilitokea Jumapili iliyopita ya Oktoba 13, mwaka huu, huko Mzambarauni, Mbagala-Charambe jijini Dar katika Kanisa la Powerful Gospel Ministry lilipo chini ya Mchungaji Meshak Punkanya ambapo Mayanga alipewa nafasi ya kutoa ushuhuda.
VIFO MILIONI 605
Mchungaji huyo alielezea kujuta kwake mbele ya kanisa kwa kudai kuwa kabla ya kuokoka alikuwa mchawi mkubwa aliyeishi kuzimu na kufanya kazi za mauaji sambamba na shetani mkuu (Lusifa) kwa kuwatumia vibaraka wake na majini.
Mchungaji Mayanga alikiri kutekeleza vifo vya watu wapatao milioni 605 wakiwemo waigizaji hao.
Steven Kanumba.
WAMO FIVE STARS, MTOTO WA DANDU
Alisema kuwa kati ya watu aliowaua kwa njia za kishirikina wamo waimbaji wa Taarab wa Kundi la Five Stars wapatao 14, Kanumba, Sharo Milionea na mwanamuziki James Dandu ‘Mtoto wa Dandu’.
Pia alidai kuwa alihusika katika vita kati ya aliyekuwa Rais wa Iraq, Sadam Hussein na Marekani kwa kutumia pepo la uchonganishi alilolitaja kwa jina la ‘Magweju’.
Pia mchungaji huyo alidai kuhusika na shambulio la hivi karibuni la Al-Shabaab katika maduka ya Westgate la Nairobi nchini Kenya na matukio mengine mengi hadi kufikia idadi hiyo ya vifo vya watu milioni 605.
Hussein Ramadhan Mkiety ‘Sharo Milionea’.
AWAONEA HURUMA WASANII, AWAONYA
Mchungaji huyo aliendelea kusimulia kuwa alipokuwa katika ulimwengu wa giza aliwahi kuwaonea huruma wasanii kama Kanumba, Sharo Milionea na Mtoto wa Dandu na kuwatokea kimiujiza akiwaonya waokoke kabla ya kuchukua roho zao huku mashabiki wao wakibaki na simanzi wakiamini kuwa vifo vyao ni vya kawaida.
Alidai kuwa baada ya kuwafuata mastaa hao na kuwaonya walikataa na badala yake akawaua.
Akiendelea kulishuhudia kanisa, Mchungaji Mayanga alisema kuwa kwa sasa ameokoka na kuachana na mambo ya giza, hivyo haogopi kuzungumza ukweli kwa kuwa roho wa Bwana anamuongoza kushuhudia kila kitu alichokifanya ili waumini watambue uwezo wa Mungu.
Gari la Sharo baada ya ajali.
ANA SIRI NZITO ZA VIGOGO
Huku akiomba hifadhi ya majina ya wahusika, mchungaji huyo alihitimisha ushuhuda wake kwa kudai kuwa ana siri nzito za vigogo au watu wakubwa ambao aliwahi kwa namna moja au nyingine kuwapa utajiri wa nguvu za giza.
UTABIRI
Hata hivyo, baadaye jamaa huyo alijitabiria kuwa atakamatwa na kufungwa siku moja kutokana na siri alizonazo.
“Yaani nina siri za watu wengi sana, nikiwaambia mtaogopa na nchi itatikisika. Najua siku moja watu watanikamata na kunifunga pingu kwa siri nilizonazo, lakini kamwe siogopi kwa kuwa Bwana ananiongoza,” alisema Mchungaji Mayanga.
Jeneza la Kanumba.
KANUMBA, SHARO MILIONEA
Kanumba alifariki dunia mwaka jana akiwa nyumbani kwake Sinza-Vatican, Dar huku Sharo Milionea akipoteza uhai kwenye ajali ya gari iliyotokea wilayani Muheza, Tanga wakati msanii huyo akienda kwao mkoani humo akitokea Dar.

JE, UNA MAWAZO GANI KATIKA HILI?TU MAONI YAKO NA USISAHAU KULIKE UKURASA WETU WA FACEBOOK

Comments

Popular posts from this blog