Waliopanda mbegu DECI hatarini kutolipwa

DeciTanzania 0acfd
WATEJA wa Kampuni ya DECI waliopanda mbegu, wanaweza wasilipwe fedha zao, MTANZANIA Jumatatu limebaini. Wateja hao ambao wanaidai kampuni hiyo Sh bilioni 39.27, huenda wasilipwe fedha zao kwa kuwa mchezo wa upatu hautambuliki kisheria. Utata huo ulijulikana mwishoni mwa wiki, baada ya Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndullu, kuzungumza na MTANZANIA Jumatatu.
"Kwanza kabisa, niseme tu kwamba hadi sasa hatujapata nakala ya hukumu hiyo ili kujua inatuelekeza nini kuhusu mchakato wa kuwalipa hao waliopanda mbegu.
"Tukipata hukumu hiyo, ndiyo tutaisoma na kufahamu tumepewa jukumu gani na gharama zitalipwa na nani katika kutekeleza mchakato huo.
"Sisi tunataka tujue hiyo hukumu inamaanisha nini, maana kwa kawaida anayechezesha na anayecheza upatu wote wana makosa, sasa utamlipaje aliyecheza?
"Lakini, kwa kuwa hatujaiona hiyo hukumu, hatujui imetuelekeza nini, lakini itakuwa ajabu kidogo kwa sababu kwa uzoefu wa nchi nyingine, waliocheza mchezo huo na waliokuwa wakiuchezesha, wote wanastahili hukumu.
"Lakini tutakachokifanya sisi, tutakaa na DPP (Mkurugenzi wa Mashtaka), ili tuweze kupata tafsiri ya sheria maana huwezi kurudi na kumzawadia fedha mcheza upatu na kumhukumu mchezeshaji," alisema Gavana Ndulu.
Akifafanua uzoefu wa nchi nyingine ambazo kesi za aina hii zimewahi kutokea, alisema fedha na mali zote za waendeshaji na wacheza upatu, huwa zinataifishwa na Serikali.
"Kesi ya DECI haikuwa ya madai bali ilikuwa ni ya jinai, na hapa nchini haijawahi kutokea kesi kama hiyo labda ndiyo maana imeleta utata. Lakini ukweli ni kwamba, suluhisho lake litapatikana baada ya kuketi na DPP na kushauriana," alisema.
Wakati Gavana Ndulu akisema hayo, wanasheria waliozungumza na MTANZANIA Jumatatu, walisema mchezo wa upatu unasimamiwa na sheria zinazosimamia upatu na kamari.
Kwa mujibu wa wanasheria hao ambao hawakutaka kutaja majina yao gazetini, sheria za upatu ziko katika michezo ya bahati nasibu na kamari ambazo zinachezeshwa kisheria kwenye Casino.
Agosti 19 mwaka huu, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Aloyce Katemana, aliiagiza Serikali kufanya mchanganuo wa mali za DECI ambazo inazishikilia kisha wateja wa taasisi hiyo walipwe.
Kesi ya DECI namba 109 ya mwaka 2009, ilifunguliwa Juni 12, mwaka 2009 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, baada ya kugundulika kuwa, kampuni hiyo ilikuwa ikiendesha mchezo huo kinyume cha sheria.
Washtakiwa katika kesi hiyo walikuwa ni Jackson Mtares, Dominick Kigendi, Timotheo Ole Loitginye, Samwel Mtares na Arbogast Kipilimba, ambao walikuwa wanatetewa na mawakili wa kujitegemea, Hudson Ndusyepo na Onesmo Kyauke.
Washtakiwa hao walikuwa wanakabiliwa na mashtaka mawili, ambayo ni kuendesha na kusimamia mradi wa upatu kinyume na kifungu cha 111A (1, 3) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16.
Wakati wa shitaka hilo, ilidaiwa kuwa, kati ya mwaka 2007 na Machi 2009, katika makao makuu ya DECI, Mabibo Mwisho, jijini Dar es Salaam, washtakiwa waliendesha na kusimamia mradi wa upatu katika sehemu tofauti nchini, kwa ahadi ya kuwapa wanachama wao fedha zaidi ambazo katika mazingira ya kibiashara ni kubwa kuliko mradi waliokuwa wakiufanya.
Shitaka la pili ni kupokea amana za umma bila kuwa na leseni, kinyume cha kifungu cha 6 (1, 2) cha Sheria ya mabenki na Taasisi za Fedha namba tano ya mwaka 2006 na kwamba, washtakiwa wote katika kipindi hicho wakiwa kwenye ofisi zao za DECI, walipokea amana kutoka kwa umma bila leseni.
DECI ilikuwa na matawi 40 katika mikoa 18 ya Tanzania Bara.
CHANZO MTANZANIA.

Comments

Popular posts from this blog