TMA yatahadharisha uwepo wa kimbunga:

Dr-Agnes-Kijazi_50bae.jpg
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk. Agness Kijazi
MAMLAKA ya Hali ya Hewa nchini (TMA) imetahadharisha kuwepo kwa kimbunga katikati ya bahari kitakachosababisha mvua nyingi za muda mfupi.
Kwa sababu hiyo mamlaka imewataka wakulima kwenye baadhi ya mikoa hasa ya kaskazini mwa nchi na iliyopo ukanda wa Ziwa Victoria kupanda mazao yanayostahimili ukame na kukomaa mapema.(P.T)
Viashiria vya vimbunga hivyo vinasababishwa na joto la bahari kupungua na hivyo kusababisha mvua nyingi za muda mfupi kwa baadhi ya maeneo.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk. Agness Kijazi, aliwashauri wakulima wa mikoa ya kaskazini mwa Dodoma, Singida na Tabora kutafuta ushauri wa maofisa ugani wa maeneo hayo kwa vile inatabiriwa kuwa na unyevunyevu hafifu kwa kipindi cha Novemba hadi Desemba.
Alitoa utabiri wa msimu wa Oktoba hadi Desemba na kuwataka wakulima wa mikoa ya Kagera, Geita, Mara, kaskazini mwa Kigoma, Arusha na Kilimanjaro kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwa sababu hali ya unyevunyevu wa ardhi utakuwepo wa kutosha.
Mkurugenzi huyo aliyataja maeneo yatakayokuwa na unyevunyevu hafifu wa udongo kuwa ni Mwanza, Simuyu, Shinyangam Manyara, Tanga, Dar es Salaam, Unguja, Pemba na Morogoro.
Akizungumzia utabiri wa msimu wa kuanzia Oktoba hadi Desemba alisema TMA inawashauri watumiaji wa taarifa za hali ya hewa wakiwemo wakulima, wafugaji, mamlaka za wanyamapori, maji na afya wazingatie utabiri huo na kutafuta ushauri wa wataalamu wa sekta husika ili kuepuka majanga.
Kwa mujibu wa Dk. Kijazi utabiri wa mamlaka hiyo kwa msimu uliopita ulifanikiwa kwa asilimia 88.2 ambapo maeneo mengi ya nchi yalipata mvua za wastani.

Comments

Popular posts from this blog