MAKAMU WA RAIS KENYA ADAI KENYA INA MARAFIKI WENGI TOFAUTI NA MAREKANI NA KAMWE HAWAWEZI KURUHUSU SERA YA USHOGA YA OBAMA

NAIBU wa Rais Bw William Ruto, jana alivunja kimya chake kuhusu hatua ya rais wa Marekani Barack Obama kutozuru humu nchini kwa kusema hatua hiyo haina madhara yoyote kwa Kenya.


Huku akiongea katika kanisa la Katoliki la St Gabriel Bahati, kaunti ya Nakuru,  Bw Ruto alisema nchi hii ina 'marafiki’ wengine wengi duniani ambao inaweza kushirikiana nao huku akiongezea kuwa hatua ya rais Obama kukwepa kutembelea Kenya haiwezi kutatiza kwa vyovyote vile uhusiano mwema uliopo wa kibiashara baina ya Marekani na Kenya.

“Tunaiheshimu nchi ya Marekani nayo inafaa kuwaheshimu Wakenya,” akasema Bw Ruto.


Alisema serikali tayari imeanzisha mikakati ya kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na mataifa  mengine  huku akikariri kuwa  safari ya Rais Uhuru Kenyatta nchini Uganda ambapo alikutana na rais wa nchi hiyo Yoweri  Museveni na mwenzao wa Rwanda rais Paul Kagame kujadili jinsi nchi hizo tatu zinaweza kushirikiana kibiashara, ni miongoni mwa mikakati hiyo.
 
“Nchi yetu inamcha Mungu na kamwe hatutaruhusu mataifa ya kigeni kutuletea tamaduni ambazo zinakinzana na desturi zetu,” akasema Bw Ruto huku akirejelea hotuba ya Rais Obama nchini Senegal ambapo aliitaka nchi hiyo kuheshimu haki za Mashoga.
Wakati mwafaka
Rais Obama ambaye yuko barani Afrika alikosa kutembelea Kenya na badala yake akazuru mataifa ya Senegal, Afrika Kusini na Tanzania; kwa kile alichokitaja kuwa haukuwa wakati mwafaka wa kutembelea nchi hii kwani viongozi wake wanakumbwa na mashtaka katika mahakama ya Kimataifa ya kupambana na uharifu wa Kibinadamu (ICC) japo aliahidi kuitembelea Kenya kabla ya kipindi chake kama rais wa Marekani

Comments

Popular posts from this blog