Kingunge azua hofu

KINGUNGE 
Na Mwandishi Wetu, RISASI Mchanganyiko
DAR ES SALAAM: Ukimya wa mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Ngombare Mwiru umezua hofu kubwa baada ya kutoonekana katika matukio muhimu tangu alipojiondoa kutoka Chama Cha Mapinduzi mwishoni mwa mwaka jana.
Kingunge alijiondoa ndani ya chama tawala, muda mfupi baada ya kukatwa kwa jina la Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na kiongozi huyo kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambako alipewa fursa ya kuwania urais wa Tanzania, akichuana na aliyeibuka mshindi, Dk John Pombe Magufuli.
“Huyu mzee yuko wapi jamani, maana yupo kimya sana, wenzake wote tunawaona na kuwasikia, wengine wanarudi CCM, wengine wanaonekana katika matukio, lakini yeye haonekani kabisa, anatupa hofu kwa kweli,” alisema msomaji aliyejitambulisha kwa jina la Giggs, akitokea mkoani Mtwara.
Msomaji mwingine, Samson Bilal wa Tabora, alisema kimya cha mwanasiasa huyo huenda kikawa na mshindo mkuu, kwani ukimya wake umekuwa siyo wa kawaida.
“Mzee Kingunge kwa kweli hasikiki kabisa, tunawasikia wenzake aliohama nao akina Msindai, Lembeli, Ole Madeye, Sumaye na hata Lowassa, lakini yeye yupo kimya,” alisema Samson.
Jitihada za gazeti hili kumsaka mkongwe huyo wa siasa za Tanzania ziligonga mwamba, baada ya kufika nyumbani kwake, Kijitonyama jijini Dar es Salaam na kushindwa kupata ushirikiano kutoka kwa watu waliokutwa, ambao pia walikataa kujitambulisha.
Wakati wa mchakato wa kumtafuta mgombea urais wa CCM mwaka 2015, mzee Kingunge alijipambanua wazi kuwa alikuwa akimuunga mkono Edward Lowassa na alikasirika baada ya jina la mtu wake huyo kukatwa, akisema hadharani kuwa taratibu zilikiukwa makusudi ili kumpata mtu aliyeandaliwa na chama hicho.

Comments

Popular posts from this blog