Aishi na risasi miaka nane


hassani akionyesha vidonda vilivyosababishwa na kulala kwamiakamingiHassani Athumani akiugulia.
Na Gregory Nyankaira, UWAZI
MARA: Ama kweli kabla hujafa hujaumbwa! Kijana Hassani Athumani (30) mkazi wa Kiabakari, Kata ya Kukirango, Wilaya ya Butiama, mkoani Mara anaishi na risasi mwilini kwa miaka nane sasa huku akiwa anasikia maumuvi makali na mwili wake ukiwa umejaa vidonda kutokana na kulala muda wote.
Kijana huyo amepata masaibu hayo baada ya kujeruhiwa kwa kupigwa risasi na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi Machi 6, 2008.
hassani akiwanamama yake mzazi pamoja namtoto wakeHassani Athumani akiwa na mama yake mzazi na mwanaye.
Akisimulia juu ya tukio hilo Ijumaa ya wiki iliyopita nyumbani kwao akiwa amelala huku akitokwa na machozi kutokana na kudhoofika mwili wake kuanzia sehemu ya mgongo aliyopigwa risasi hadi miguuni, Hassani alikuwa na haya ya kusema:
“Hiyo Machi sita mwaka 2008 tulikuwa tunacheza disko na wenzangu katika ukumbi mmoja uliopo Kiabakari, ghafla saa 4.30 usiku, majambazi yakiwa yamevalia makoti meusi na kufunika nyuso zao, yalivamia katika ukumbi huo na kuamuru wote tulale chini kisha wakaanza kurusha hovyo risasi, ambapo risasi mbili zilinipata moja ikaingia mgongoni na nyingine ikaniparaza kichwani.
 “Baada ya kupigwa risasi hizo, nilianguka na kupoteza fahamu na nilipopata fahamu nilijikuta nikiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Mara mjini Musoma ambako nilipelekwa na wasamaria wema ambako nilitibiwa kwa siku mbili kisha kuhamishiwa katika Hospitali ya Rufaa Bugando jijini Mwanza kwa matibabu zaidi.
“Nilikaa Bugando kwa miezi sita bila kupona na kushauriwa na madaktari wa hospitali hiyo kuwa hawana uwezo wa kuondoa risasi mgongoni badala yake niende nchini India, nilishindwa kwenda huko kwa sababu ya ukosefu wa fedha na nikarudishwa nyumbani ambako naendelea kuteseka hadi leo nikiwa na risasi hiyo mwilini kwa miaka nane sasa.
hassani kabla yakupigwa risasi Hassani Athumani kabla hajapigwa risasi.
“Niliambiwa na madaktari kwamba risasi iliyoingia mgongoni iliingia ndani ya uti wa mgongo na kukata mishipa yote ya fahamu na tangu siku hiyo ya tukio nimelemaa moja kwa moja kuanzia eneo ilipoingia risasi hadi miguuni.
“Nimekuwa mlemavu wa miguu bila kutarajia, sina matumaini yoyote ya kurudia hali yangu ya mwanzo maana mwili umeingia ganzi na miguu imekuwa myembamba kabisa, sina fedha ya kwenda India, sasa nimejikabidhi kwa Mungu, sijui nilikosa nini kwa muumba wangu hadi kupewa adhabu hii!
“Najiuliza kila kukicha nani atanitunzia mtoto wangu ambaye mama yake alishafariki, kwetu hatuna uwezo, sina baba nina mama pekee anayeishi kwa kuuza samaki wa kukaanga, najisaidia haja kubwa na ndogo hapa nilipolala, sina uwezo wa kuamka, mama yangu kila wakati ananibadilishia matandiko kama mtoto mchanga…,” alishindwa kujieleza Hassani akawa analia kwa kwikwi!
Mgonjwa huyo ana vidonda sehemu kadhaa za mwili kutokana na kile alichosema kulala kwa muda mrefu kwa kuwa huwa anashindwa kujigeuza.

Comments

Popular posts from this blog