Mrembo abakwa, auawa!

auawaMrembo Sijaona Issa
Na Gladness Mallya, RISASI MCHANGANYIKO
CHALINZE: Inauma sana! Mrembo Sijaona Issa (25) mkazi wa Pela, Chalinze mkoani Pwani, amebakwa na kuuawa kikatili na watu wasiojulikana, ingawa yapo madai ya wivu wa kimapenzi.
Akizungumza kwa uchungu, mama mzazi wa marehemu alisema kuwa tukio hilo lilitokea wiki iliyopita baada ya wasamaria wema kukuta mwili wa mwanaye umelazwa uwanjani ukiwa umefunikwa na kanga moja.
AUAWA (1)Mama wa Marehemu
“Jumanne jioni marehemu alirudi kutoka kazini saa tatu usiku, akala chakula kama kawaida na kuingia chumbani kwake na sikujua kama alitoka mpaka asubuhi ya saa moja Alhamisi, ambapo kuna kijana alikuja na kuniuliza kama marehemu yupo ndani, nikaenda chumbani kwake sikumkuta, nilikuta tu nguo zake alizotoka nazo kazini na viatu.
“Baada ya kurudi na kumwambia hayupo ndipo huyo kijana alisema amekutwa ameuawa uwanjani karibu na Tanesco, ndipo kaka yake akaenda kumuangalia na kukuta kweli ni yeye,” alisema mama huyo.
AUAWA (2)
Waombolezaji
“Mwanangu alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na kijana mmoja (jina linahifadhiwa) lakini miezi kadhaa iliyopita marehemu alishindwana na kijana huyo kutokana na kudai ana wivu sana kwani alikuwa akimpiga kila siku, siku moja aliwaita wajomba zake na kuwaambia kwamba hamtaki tena huyo mtu.
“Kijana aliposikia hivyo palepale alitoa kauli kwamba kama amemkataa atamfanyia kitu ambacho hatakisahau katika maisha yake, hivyo hata siku hiyo walienda kuonana usiku huo na tunaamini huyo kijana ndiye katekeleza mauaji hayo kwani alishaahidi,” alisema mama huyo.
Mama huyo aliiomba serikali kuchunguza vizuri mauaji hayo kwani mwanaye alifanyiwa unyama mkubwa, ikiwa ni pamoja na kutobolewa macho, kuvunjwa bega na kunyongwa.
Naye Mwenyekiti wa Pela na mji mdogo wa Chalinze, Hussein Mramba alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa mwili wa marehemu ulionekana kuwa na majeraha kama shingo kuvunjwa, bega kisa kikidaiwa kwamba kulikuwa na mgogoro wa kimapenzi na mpenzi wake.
“Ni kweli tukio hilo limetokea na ninaahidi kuwa niko bega kwa bega na familia pamoja na jeshi la polisi ili kuhakikisha wauaji wanajulikana na kukamatwa,” alisema mwenyekiti huyo.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani, Boniventura Mushongi hakupatikana kupitia simu yake ya mkononi ili azungumzie suala hilo, kwani iliita kwa muda wote bila kupokelewa. Marehemu alizikwa Alhamisi iliyopita katika Makaburi ya Msuwa yaliyopo kijijini hapo.

Comments

Popular posts from this blog