Mume amfunga mkewe mtini kisa kutopata mimba


DSC02365
Jeni Marwa akiwa amefungwa kamba mtini na mumewe.
Stori: Gregory Nyankaira, UWAZI
MARA: Nyango Hakimu mwenye umri wa miaka 37, anatafutwa na polisi akidaiwa kumfunga mkewe Jeni Marwa (23) kwenye mti na kumpa kichapo kilichomsababishia majeraha kwa madai ya kutoshika ujauzito kwenye ndoa yao.
Tukio hilo lilitokea jioni ya Februari 6, mwaka huu katika Kijiji cha Singu, kilichopo Kata ya Kukirango wilayani Butiama mkoani Mara, ambako mwanamke huyo alipigwa kwa fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake, akidaiwa kutokuwa na faida nyumbani hapo.
Mashuhuda wa tukio hilo wamesema, baada ya mumewe kumfunga mkewe kamba mikononi na miguuni kabla ya kumfunga kwenye mti na kuanza kumchapa, mwanamke huyo alipiga mayowe ya kuomba msaada ndipo watu walifika na kumkuta akitokwa damu nyingi baada ya kukatwa na kisu mguuni.
DSC02366
Huku mumewe akiwa amekimbilia kusikojulikana, wasamaria wema walimchukua na kumpeleka Kituo cha Polisi cha Kiabakari ambako alipewa fomu ya matibabu (PF3) kabla ya kupelekwa Zahanati ya Mwanza Buriga kwa matibabu, ambako baada ya kutibiwa, alirudi kwa wazazi wake akisubiri hatua zaidi za kisheria.
Watu wa karibu wa wanandoa hao wamedai kuwa mwanamke huyo amewahi kurejeshwa kwao mara nane ambako alikabidhiwa kwa wazazi wake mbele ya viongozi wa kitongoji huku mumewe akisema hamtaki, lakini mara zote hizo wazazi wa mwanamke wamekuwa wakimtaka kurejea kwa mumewe kwa kile kinachodaiwa kukosa mahari ya kurudisha, ambayo ni ng’ombe watano.
Akizungumza na Uwazi akiwa katika zahanati hiyo ya Mwanza Buriga, Jeni alisema: “Tangu niolewe nimekuwa mtu wa kupigwa na mateso ya kila siku kisa kikiwa kutoshika ujauzito.”
Polisi wa Kituo cha Kiabakari wamethibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kwamba wanasubiri kuletewa PF3 hiyo kwa hatua zaidi za kisheria.

Comments

Popular posts from this blog