LICHA YA KUSHUTUMIWA KATIKA SAKATA LA ESCROW MUHONGO AKEMEA RUSHWA TANESCO

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akizungumza na wananchi wa kijiji cha Surubu, Kata ya Komaswa wakati wa ziara yake wilayani Tarime Mkoa wa Mara.Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amewataka wananchi wa vijiji vya wilayani hapa kutoa taarifa za mianya ya rushwa wakati wanapoomba kuunganishiwa umeme majumbani.Muhongo alisema hayo juzi alipokuwa akikagua awamu ya pili ya Mradi wa Umeme Vijijini unaoendelea kwa nchi nzima na ambao mkoani Mara unatekelezwa katika vijiji 197.Alisema katika mradi huo, Serikali haitamwonea huruma mfanyakazi yeyote wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) atakayebainika kuomba rushwa ili atoe huduma.
“Msitoe hongo,” alisema Profesa Muhongo. “Kati ya vitu ambavyo Serikali haitaki kuvisikia ni rushwa. Msidanganywe kuwa mkitoa rushwa ndiyo mtarahisishiwa kupata umeme kwa haraka.”
Alisema gharama zote za kuunganishiwa umeme kwa mwanakijiji zinalipwa na Serikali na kiasi cha Sh27,000 ni tozo ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (Vat).
Baadhi ya watu walilalamika kuwa mradi huo unawanufaisha wakazi wachache walio jirani na barabara zinakopita nguzo za umeme na kuacha maeneo yaliyo na watu wengi na huduma za kijamii kama shule na zahanati.
“Huduma inayotolewa na ofisi za Tanesco katika wilaya hii ni mbovu sana na mradi huu unapita mbali na makazi ya wanakijiji wengi. Tunaomba utusaidie ili tupate huduma bora,” alisema mkazi wa Bunda, Sherida Charles.
Naye kaimu mkuu wa wilaya hiyo, Angelina Mabula aliwataka wananchi kuchangamkia fursa hiyo ya kuunganishiwa umeme ambayo alisema ni chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali hasa ya afya na elimu.
“Hivi sasa kuna ujenzi wa maabara za kisasa katika shule zetu, haziwezi kufanya kazi bila umeme,” alisema Mabula.
Mabula alisema vikiunganishiwa umeme, vituo vya afya vitaondokana na adha ya wauguzi kuhangaika na vibatari wanapotoa huduma, hususan kwa wajawazito.
“Watakuwa pia wamejikomboa kutembea umbali mrefu kutafuta huduma bora na salama na hakutakuwa na haja ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo,” alisema Mabula.
Aidha aliwataka wananchi kulinda miundombinu ya umeme hasa wale walio zoea kuiba mafuta ya Transifoma na nyaya kwa makusudi ya kuuhujumu uchumi wananchi

chanzo:gazeti la mwananchi

Comments

Popular posts from this blog