ZSTC yastawisha upya zao la karafuu, Zanzibar.




 Zanzibar ni visiwa vinavyosifika kwa uzalishaji wa karafuu bora duniani. Katika miaka 30 ya nyuma pia ilisifika kwa uzalishaji karafuu nyingi, wastani wa tani 8,605 zilikuwa zikizalishwa kwa mwaka.

Jamii ya wakati huo walikuwa wakizijali, wakizithamini na wakizipenda sana karafuu ukilinganisha na kizazi cha sasa. Walihakikisha karafuu zao wakiuza vituoni tena zinakuwa safi, zimekauka vizuri na zinapata daraja la kwanza.

Katika miaka hiyo zao la karafuu lilikuwa ndiyo tegemeo kubwa la pato la kiuchumi katika visiwa vya Zanzibar.  Pato la Serikali lilitegemea sana zao hilo na kuiwezesha kuenedesha mipango yake ya kiuchumi na kijamii bila ya kuyumba. Hali hiyo ilitokana na ukubwa wa soko la dunia na ubora wa kipekee wa karafuu za Zanzibar katika soko hilo.

Lakini kwenye miaka ya 1990, hali ya soko haikuwa nzuri sambamba na kushuga kwa bei na kuongezeka kwa nchi zinazozalisha karafuu duniani na hivyo kuleta ushindani wa kibiashara.

Kushuka kwa bei katika soko la dunia kulipelekea kushuka kwa ari ya  uzalishaji kwa wakulima na kupelekea visiwa vya Zanzibar navyo kupoteza muelekeo wa zao hili. Zao hili lilipoteza hadhi yake ya kuwa zao la uchumi wa nchi.




Wakulima wengi waliacha kulima zao la karafuu na badala yake walijihughulisha na mazao mengine ukiwemo ukulima wa mwani ambapo wakati huo ulionekana kama ungelikuwa mbadala wa zao la karafuu.

Lakini pamoja na kuyumba kwa soko la dunia, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, iliendelea kununua karafuu kutoka kwa wakulima, ingawa si kwa bei ya kiwango cha juu. Serikali ililazimika wakati mwengine kufidia gharama za bei katika kuona mkulima ambaye ni mwananchi anaendelea kujenga imani na kulithamini zao la karafuu.

Wanafalsafa ya kiswahili wanao msemo usemao baada ya dhiki faraja, hivyo ndivyo ilivykuwa kwa wakulima wa karafuu baada ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kupandisha bei ya zao hili kufuatia kutengemaa kwa hali katika soko la dunia mwaka 2011.

Serikali iliamua kupandisha bei hadi kufikia shilingi 15,000 kwa kilo kabla ya kushuka kidogo kutokana na kutegemea kupanda na kushuka kwa bei katika soko la dunia.

Aidha katika mwaka 2011 ZSTC ilimeongeza bei ya karafuu kutoka 3500/- hadi 10000/-  na baadae kuongezwa tena hadi 14,000/- kwa kilo. Mkulima analipwa asilimia 80 ya bei inayouzwa nje ya nchi.
Baada ya Serikali kuliimarisha Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC), hali ya ustawishaji wa zao la karafuu ilianza kurejea na wakulima walianza tena kulistawisha zao hilo. Mtazamo chanya wa ZSTC kwa kiasi kikubwa umeweza kurudisha hadhi ya zao la karafuu ya Zanzibar kuanzia kwa wakulima na hata katika soko la dunia.




ZSTC chini ya Mkurugenzi Muendeshaji Bi. Mwanahija Almas Ali imekuwa mstari wa mbele hivi sasa kuhakikisha hadhi ya karafuu ya Zanzibar inarejea katika sifa yake ya asili kwa kushirikiana na wadau wa zao hilo wakiwemo wakulima.                           


Kiujumla, karafuu ni zao pekee la kilimo ambao linaiingiza fedha nyingi za kigeni, ambapo serikali imetoa kipaumbile kwa zao hilo katika kukuza uchumi Zanzibar pamoja na ustawi wa wananchi wake.
Jitihada kubwa zinachukuliwa na serikali katika kuhakikisha kiwango cha uzalishaji, usafirishaji na ubora wa karafuu za Zanzibar unaimarika kwa kushirikina na wadau wote wa zao hili wakiwemo wakulima, wafanya biashara, Serikali za Wilaya na Mikoa na Taasisi za ulinzi na usalama.      

Miongoni mwa mambo ambayo yaliofanywa na serikali katika jitihada za kuimarisha zao la karafuu ni pamoja na kuongeza bei ambapo mkulima anapata asilimia 80% ya bei inayouziwa karafuu nje ya nchi.
Kutoa miche bure kwa wakulima ili kuongeza idadi ya miti ya mikarafuu visiwani sambamba na kujengwa vituo karibu na maeneo ya wananchi kwa kurahisisha usafirishaji wa karafuu kutoka sehemu waliopo hadi vituoni.

Kuanzisha mpango wa kuifanya karafuu ya Zanzibar ijulikane dunia nzima kutokana na sifa zake za kipekee kupitia mradi wa tasnia bunifu (BRANDING).  Kuifanya karafuu kuwa chini ya umiliki wa serikali kwa lengo la kumjengea mkulima uwezo wa kimaslahina kumuongezea ari ya kulipenda zao la karafuu.




Kujenga vituo vipya vya manunuzi karibu na wakulima ili kurahisisha shughuli za usafirishaji wa karafuu mfano hivi sasa Pemba kuna vituo zaidi ya 30 na Unguja kuna vituo zaidi ya sita ingawa hivi sasa Unguja kituo kinachofanyakazi ni kimoja kilichokuwepo tangu miaka ya zamani, tofauti ni kwamba kituo cha zamani kwa Unguja kilikuwepo Malindi na cha hivi sasa kipo Saateni.


Kuongeza idadi ya vituo ni moja ya juhudi za Serikali kuwapunguzia gharama za usafiri wananchi wake pamoja na kuwaondolea usumbufu ambao sio wa lazima. 
Kuanzisha vituo vya uatikaji miche ya mikarafuu, kununua miche ya mikarafuu kutoka kwa wakulima walioanzisha vituo na kupatiwa bure miche hio wakulima.  Kila mwaka zaidi ya miche 1,000,000 inazalishwa na kugaiwa bure kwa wakulima. Jitihada hizi zimeanza zamani na bado zinaendelea.

Karafuu za Zanzibar zina sifa kubwa duniani ukilinganisha na karafuu zinazozalishwa na nchi nyengine ambazo zinazalisha kwa wingi zaidi ukilinganisha na Zanzibar.Sifa hiyo inahitaji kulindwa , Serikali hivi sasa imeandaa mkakati wa kuilinda karafuu ya Zanzibar mkakati ambao utawakwamisha wale wote watakaojaribu kuharibu sifa hiyo.

Sifa nzuri za kiwango cha juu cha kipekee cha karafuu ya Zanzibar ni ukaukaji wake, usafi wake ladha yake na haiba yake ya kimaumbile ambapo viwango hivi vinafahamika katika soko la dunia tangu miaka 50 iliyopita na vinaendelea kutumika hadi hii leo.

Sifa hiyo ya karafuu inajengwa na wadau wote wenye kujishughulisha na zao hili, hivyo haitokuwa vyema kufanya makosa ambayo yatapoteza ubora wa karafuu ya Zanzibar, ikwemo kuanika barabarani na kuzichanganya na uchafu usiohitsjika ikiwemo makonyo, matende au udanganyifu mwengine.

Jambo la msingi ni kuongeza mashirikiano ya pamoja kati ya Shirika,Wakulima na wadau wote wa zao la karafuu katika kuongeza kiwango cha uzalishaji, usafirishaji na ubora wa karafuu za Zanzibar.

Comments

Popular posts from this blog