MCHUNGAJI AFUNGUKA JUU YA FLORA MBASHA NA MUMEWE..!


 Mbasha akiwa na Pingu.
WAKATI mume wa mwimba Injili Bongo,  Flora Mbasha, Emmanuel Mbasha akiachiwa huru kwa dhamana kufuatia kesi ya kudaiwa kumbaka shemejiye, Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima la jijini Dar es Salaam, Josephat Gwajima ameibuka na kunena mazito kuhusiana na sakata hilo, Risasi Jumamosi limesheheni mkobani.
Mbasha aliachiwa kwa dhamana juzi akitokea Gereza la Keko, Dar baada ya kupandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Juni 17, mwaka huu na kusomewa mashitaka mawili ya ubakaji ambayo hata hivyo, aliyakana.

Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima la jijini Dar es Salaam, Josephat Gwajima.
 ILIVYOKUWA KORTINI
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, mheshimiwa Wilbeforce Luago siku hiyo ya Juni 17, alitoa hoja kwamba upande wa jamhuri hauna pingamizi hivyo dhamana ipo wazi.


Emmanuel Mbasha akielekea kizimbani.
 Alisema mshitakiwa alitakiwa kuwa na wadhamini wawili, mfanyakazi wa serikali na wa kutoka katika taasisi inayotambulika sanjari na shilingi milioni 5 kila mmoja. Mshitakiwa alishindwa kutimiza masharti hayo siku hiyo hadi hadi juzi alipotimiza, akaachiwa.

Mume wa mwimba Injili Bongo,  Flora Mbasha, Emmanuel Mbasha akiwa chini ya ulinzi.
 Mwendesha mashitaka wa mahakama hiyo ambaye ni wakili wa serikali, Nassoro Katuga bila kuchelewa aliitaja kesi hiyo yenye namba CC/186/2004 ambapo rafiki wa Mbasha aliyejitambulisha kwa jina la George Mushi na baba wa mtuhumiwa aitwaye Mwahimu Juma ndiyo waliofanikisha dhamana hiyo. Kesi yake itatajwa tena Julai 17, 2014.

Bw. Emmanuel Mbasha akiondoka baada ya kupewa dhamana.

GWAJIMA SASA
Akizungumza na paparazi wetu juzi wakati Mbasha akiwa nje kwa dhamana, Mchungaji Gwajima alieleza namna ambavyo sakata hilo limeitikisa Injili nchini Tanzania kutokana na kuibuka kwa madai mengi likiwemo suala la Flora kusemekana amehamia nyumbani kwake kitu ambacho alikipinga.

Gwajima alisema anasikitika sana kuona ndoa ya Flora na Emmanuel Mbasha inatikisika akizingatia Flora ni muumini wake hivyo moja kwa moja ugomvi wao unaonekana kutia dosari mwenendo mzima wa uinjilishaji katika jamii. 
“Naumizwa sana na sakata hili lakini hivi karibuni niliamua kuwaita ndugu wa pande zote mbili (Flora na Mbasha) nikazungumza nao kwa kirefu na tukamaliza tofauti zote lakini tatizo likabaki lile la kisheria zaidi (mashitaka ya ubakaji kwa Emmanuel),” alisema Gwajima ambaye makao makuu ya kanisa lake yapo Kawe jijini Dar. 
AANDAA TAMKO ZITO
Mchungaji Gwajima alisema kutokana na sakata hilo kugusa Injili, ameandaa tamko zito ambalo atalitoa rasmi atakaporudi safari yake ambayo hakueleza anakokwenda.
“Hatuwezi kukaa kimya juu ya hili, nasafiri lakini nikirudi tu nitatoa tamko rasmi kwa kuwaalika waandishi wa habari,” alisema.
 

IBADANI JUMAPILI
Katika hatua nyingine, ndani ya ibada ya kanisa hilo iliyofanyika Jumapili iliyopita, Mchungaji Gwajima alitumia dakika kama 15 katika mahubiri yake kutupa kile kilichodaiwa kuwa ni jiwe gizani ambapo wengi waliamini ni kuhusiana na sakata hilo.
 
“Mimi siyo kama wale, sijibu hoja kama zile, mfano ukiwa unaoga halafu chizi akachukua nguo zako na ukamkimbiza nani ataonekana chizi? Tatizo la Watanzania ni kuwa wakisikia kitu kipya kinaanza kwao badala ya kukithamini wanakididimiza ili kisiendelee, lakini mimi siyo kama wao,” alisema.
Aliongeza: “Mimi kila mwaka naenda Japan na ninawa-lecture Wajapani ambao pia huja hapa kanisani zaidi ya 40 kila mwaka na mwaka huu watakuja Septemba, lakini Watanzania hawashtuki na kuja kujifunza juu ya ufufuo wa wafu wengi wao wanakalia kuandika stori kwenye magazeti lakini mimi siyo kama wale.” 

AMEFUNGUKIA SAKATA LA MBASHA?
Ingawa Mchungaji Gwajima hakueleza moja kwa moja kuhusu tukio la Mbasha lakini maneno hayo yalitafsiriwa kwamba ni ya kujibu hoja zinazomhusisha yeye na tukio hilo.
Anaendelea:”Mimi nimehubiri nchi zaidi ya 53 duniani na nyingi za Ulaya na Marekani halafu mtu amekaa Magomeni miaka yote anatengeneza stori ya gazeti, unatarajia niijibu, mimi siyo kama wale nimetumwa na nina kazi natakiwa kuifanya duniani na siwezi kufa mpaka niimalize.”

Ndugu na jamaa wa Emmanuel Mbasha waliofika mahakamani.
 AYAGEUKIA MAGAZETI
“Inawezekana mlishawaangamiza wengi kabla ya mimi, kwa kuwatungia stori hizo za uongo lakini mimi siyo kama wale na mwezi huu wa nane ninaendelea na mkutano Iringa, waache waandike lakini mimi ni chombo kingine na siyo kama wale.”
  
DONGO GIZANI?
Baadhi ya waumini waliokuwa katika ibada hiyo, walibaki njia panda na katika giza nene ingawa wengi waliamini alitupa vijembe katika sakata la Mbasha haswa alipokuwa akisema, ‘mimi siyo kama wale’.
ILIWAHI KUANDIKWA
Katika Gazeti la Uwazi, toleo la Juni 10, 2014  kulikuwa na habari ukurasa wa mbele ikiwa na kichwa; Mbasha: Gwajima nianchie mke wangu.
 

Katika habari hiyo, Mbasha alishangazwa na kusikia habari kwamba, baada ya kutofautiana na mke wake na kutokea madai ya kumbaka shemeji yake, mkewe alihamia nyumbani kwa Gwajima kujisitiri lakini madai hayo, Gwajima aliyapinga vikali. Baadaye ilibainika kuwa, Flora anaishi hotelini Sinza, Dar.

Comments

Popular posts from this blog