MTALII ALIYEKWAMA KILELE CHA MAWENZI MLIMA KILIMANJARO AOKOLEWA.

Mtalii Jeanne Traska kutoka Ujerumani
Bi.Jeanne Traska kutoka Ujerumani na Muongoza Wageni Athumani Juma wakiwa katika Lango la Marangu pamoja na vifaa mbalimbali walivyokwama navyo katika kilele cha Mawenzi Mlimani Kilimanjaro mara baada ya kuokolewa.

Kikosi cha Uokoaji katika Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro kimefanikiwa kumuokoa mtaliiBi. Jeanne Traska (32) kutoka Ujerumani pamoja na muongoza wageni Athuman Juma ambao jana walikwama katika kilele cha Mawenzi Mlimani Kilimanjaro. Kikosi cha Uokoaji cha TANAPA kiliweza kufika eneo la kilele cha Mawenzi na kwa kutumia mbinu za uokoaji za kisasa kabisa kiliweza kuwanasua majira ya kumi na moja jioni.

Licha ya hali mbaya ya hewa iliyotokana na mawingu mazito katika eneo hilo, Kikosi cha Uokoaji cha TANAPA kiliweza kukabiliana na hali hiyo na kuweza kuwanasua na kisha kuwapeleka katika kituo cha Horombo majira ya saa mbili usiku ambapo walichukuliwa na gari kupitia njia maalum ya uokoaji na kufika katika Lango Kuu la Marangu saa nne na nusu usiku.

Hali ya hewa ilisababisha helikopta
maalum iliyoletwa kwa ajili ya zoezi la uokoaji kushindwa kufanya kazi kwa kuwa mawingu mazito hayakuwezesha marubani kuliona eneo la kilele kwa urahisi.
Hivi sasa mtalii huyo pamoja na muongoza wageni wake bado wapo chini ya uangalizi wa hifadhi kwa kushirikiana na Kampuni ya Nordic Tours iliyomleta mgeni huyo.

Aidha, kwa kuwa ni tukio lisilo la kawaida, uongozi wa hifadhi unaendelea kuchunguza sababu zilizowafanya kuchepuka njia na kuelekea kilele cha Mawenzi badala ya Kibo. Kwa kawaida Kilele cha Mawenzi huwa hakitumiwi na watalii isipokuwa kwa kujaza fomu maalum inayoonyesha kuwa mgeni amekubali kwa hiyari yake kupanda kilele hicho.

Imetolewa na
Idara ya Mawasiliano
Hifadhi za Taifa
Tanzania
23.03.2014

Comments

Popular posts from this blog