ZIFAHAMU VYEMA NJIA YA KUAMSHA NA KUZITEKA HISIA ZA MPENZI WAKO

NAAMINI rafiki zangu wote mtakuwa wazima wa afya njema, kama mimi na mpo tayari kuanza darasa hili jipya baada ya kumaliza somo lililopita last week. Karibuni tujifunze pamoja na ninaomba utayari wako ili uweze kuingiza kitu kipya ubongoni mwako.


HISIA NI NINI HASA?
Katika tafsiri ya kawaida hisia ni neno linalotokana na hisi, fikiri, buni. Kwenye uwanja wa mapenzi linanyambulishwa tofauti kabisa. Huku linajulikana kama mshawasha, mhemko, miliki n.k.
  

                           
Mara nyingi nimekuwa nikisisitiza kwamba, mapenzi ni furaha na kama upo kwenye uhusiano ambao una mateso na kila aina ya matatizo, basi ujue kwamba haupo sahihi. Hakuna masimango kwenye mapenzi, kunyanyasana na maumivu.

Tafsiri hasa ya mapenzi ni upendo, sasa kama ndivyo, si sahihi kuwa kwenye upendo, halafu chuki inachanganyika ndani yake. Hayo niliyoyataja hapo juu, mama yake ni chuki! Ndugu zangu, nirejee kusema tena kwamba uwanja wa huba ni mpana sana na unahitaji elimu kila wakati.

Wakati naandika mada hii ofisini, nilipata ugeni wa dharura. Nilipigiwa simu kutoka Mapokezi na kuelezwa kwamba nina wageni muhimu sana wanaonihitaji. Niliacha kwanza kuandaa mada hii na kuagiza waingizwe kwenye chumba cha mahojiano, kisha nikaenda.

Walikuwa wasichana wawili, ambao walionekana kuwa ni marafiki. Kwa kawaida huwa nakutana na wasomaji wangu (kwa mambo ya ushauri) kila Jumapili kwa kuweka ahadi maalumu, hivyo ujio wao haukunifanya nihisi kwamba walikuwa na shida ya mambo ya mapenzi.

Kwa haraka nikajua kwamba walikuwa na mambo mengine ya kihabari, lakini nilipowauliza, wakasema kwamba mmoja wao alitaka kuzungumza nami kwa kuwa alikuwa na hali mbaya sana katika uhusiano wake. Nikawapa utaratibu kuwa waje kuniona Jumapili (keshokutwa).

Pamoja na kuwapa utaratibu huo, waliomba sana kuzungumza nami kwa vile, mmoja wao alikuwa na tatizo kubwa. Haikuwezekana, nikamshauri nimpatie namba yangu maalumu ambayo angenipigia kwa muda niliompangia, hapo akasema: “Simu? Sawa, lakini tatizo ni kwamba ukinipigia atapokea... (mpenzi/mchumba/mume wake) simu yangu amei-divert kwake. Mh!

Anyway, nitakupigia huo muda.”
Tukaachana kwa ahadi kwamba angenipigia siku hiyo kwa muda ambao tulikubaliana.

TUNAJIFUNZA NINI?
Pamoja na kwamba sikuweza kuzungumza naye chochote mpaka naandika mada hii, niligundua mengi sana kutoka kwa dada yule ambaye kwa haraka nilimkadiria kuwa na umri kati ya miaka 22-28.

Ni msichana mrembo kwa kumtazama, lakini uso wake umepoteza matumaini. Anaonekana yupo kwenye uhusiano ambao kwake ni mateso. Nathubutu kusema kwamba, inawezekana kabisa yupo kwenye mapenzi ya utumwa.

rafiki zangu, inapofikia hatua mpenzi wako hakuamini kiasi kwamba ana-divert simu yako kwake, ujue hapo kuna tatizo. Niliagana na dada huyo nikimpa matumaini makubwa kwamba, tatizo lake lingeisha kwa kuwa hakuna kisicho na dawa.

Nilimwambia: “Samahani nashindwa kuongea na wewe sasa hivi kwa kuwa ni nje ya utaratibu, lakini pia nina majukumu mengi yanayonisubiri, ila nakuhakikishia tatizo lako limefika mwisho. Kwa kuwa umeonana na mimi, amini masaibu yako yameshapata dawa!”

Nashukuru aliondoka akitabasamu kidogo. Nilikuwa na matarajio makubwa ya kumpa dawa ya tatizo lake. Wiki ijayo nitawaletea mrejesho. Rafiki zangu, niliona hili liwe kama utangulizi wa somo letu.

HISIA NI NINI HASA?
Katika tafsiri ya kawaida hisia ni neno linalotokana na hisi, fikiri, buni. Kwenye uwanja wa mapenzi linanyambulishwa tofauti kabisa. Huku linajulikana kama mshawasha, mhemko, miliki n.k.

Kwa kifupi, hakuna tafsiri ya moja kwa moja ya neno hilo, lakini limebeba ile hali ya mwenzi kuwa na hamu, mapenzi, uhitaji zaidi kwa mwenzake. Ndiyo maana mtu anaweza akauliza, “Nitawezaje kuteka hisia za mpenzi wangu?”
Bila shaka tupo pamoja.

UNAZITEKAJE?
Hapo ndipo kwenye tatizo kwa watu wengi walio kwenye uhusiano. Wapo wasioweza kabisa kuteka hisia za wapenzi wao. Hawajui mbinu za kufanya hivyo. Rafiki zangu, suala la kumfanya mpenzi wako akupende, awe na hamu na wewe, akufikirie, asiwaze kukusaliti lipo mikononi mwako.

Ni kazi yako. Hapo unaanza na kujua ni mambo gani ambayo hayapendi na yapi anayapenda. Kujua jambo hilo, unakuwa unaelekea kwenye kuelewa namna ya kumaliza kabisa tatizo hilo.
Kuna ambao wapo kwenye uhusiano, halafu wanashangaa ghafla wapenzi wao wamebadilika.

Wanakuwa wakali bila sababu, wakorofi, hawana hamu ya kukutana nao faragha na mengine. Umewahi kujiuliza kwa nini? Jibu ni rahisi sana, AMEPOTEZA HISIA KWAKO!
Kama ndivyo, kazi ipo mikononi mwako ya kurejesha hisia hizo kama zamani. Yapo mambo mengi ambayo natakiwa kuzungumza na wewe kuhusu namna ya kurejesha hisia za mwenzi wako kwako. Ni rahisi sana, wiki ijayo nitakuletea.

Kitu kikubwa rafiki yangu, ninachotaka kukuacha nacho ni kwamba, matatizo mengi kwenye uhusiano husababishwa na kupoteza hisia. Mchunguze mpenzi wako, siku hizi anakukaripia? Anakusimanga? Hakusikilizi?

Anakudharau? Hapendi kukushirikisha kwenye mambo yake? Kama una matatizo haya ujue chanzo chake ni kupoteza hisia. Kazi yangu mimi ni kurejesha amani katika uhusiano wako, wiki ijayo si ya kukosa rafiki zangu. Naweka nukta.

Comments

Popular posts from this blog