WANANCHI WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA ZA ELIMU

Rc Dsm
Na Aron Msigwa – MAELEZO,  Dar es salaam.
Serikali imewataka wananchi kuzitumia ipasavyo fursa za elimu zinazotolewa kupitia programu mbalimbali za ikiwemo Elimu ya Watu Wazima (EWW) na ile ya Elimu Nje ya Mfumo Rasmi (ENMRA) ili kupunguza tatizo la umasikini, maradhi na ujinga.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es salaam na Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Bw. Said Meck Sadiki wakati akitoa taarifa kwa wananchi wa mkoa wa Dar es salaam kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Elimu ya Watu Wazima na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi yatakayofanyika jijini Dar es salaam kuanzia Novemba 13, 2013 yakiongozwa na kauli mbiu “Kisomo kwa ajili ya Karne ya 21”
Amesema  serikali imeanzisha programu mbalimbali za elimu kuanzia msingi mpaka sekondari kwa lengo la kuwawezesha wananchi kupata fursa hiyo na kuondokana na tatizo Umaskini, maradhi na ujinga na kuwawezesha kujikwamua  kiuchumi, Kijamii, Kisiasa na Kiutamaduni.
Ameeleza kuwa mkoa wa Dar es salaam kwa sasa unaratibu program mbalimbali zikiwemo Mpango wa Elimu ya Msingi kwa walioikosa (MEMKWA) unaowahusisha wanafunzi wenye umri kati ya miaka 9 hadi 18 ambao husoma katika mfumo wa makundi rika.
Amesema  jumla ya wanafunzi 1,846 wamejiunga na program hiyo kwa mwaka 2013 wakihusiha wale wenye umri wa miaka 9 mpaka 13 na 14 mpaka 18.
Bw. Meck Sadiki ameeleza kuwa mkoa wa Dar es salaam pia unasimamia Mpango wa Uwiano kati ya Elimu ya Watu Wazima na Jamii (MUKEJA) unaohusu utoaji wa Elimu kupitia kisomo cha kujiendeleza na kisomo chenye manufaa kinachowahusisha watu wazima wenye umri zaidi ya miaka 18 wapatao 1,678 waliojiunga kwa mwaka 2013.
Ameongeza kuwa wanafunzi wapatao 2,309 wamejiunga na programu ya Elimu ya Sekondari Huria (PESH) ambayo huendeshwa kwa wanafunzi ambao wamekosa sifa za kuchaguliwa kujiunga na shule za sekondari kupitia chaguo la mfumo rasmi.
“Wanafunzi wanaosoma katika mpango wa PESH serikali imewawekea utaratibu wa kusoma katika shule za msingi na sekondari ambazo hazina utaratibu wa awamu mbili za kusoma, wao husoma jioni baada ya muda wa kawaida wa masomo”
Aidha amezitaja programu nyingine za elimu zinazowahusisha watu wazima  na vijana kuwa ni pamoja na Elimu ya Masafa na Ana kwa Ana (ODL) ambayo ina jumla ya wanafunzi 335 wanaoendelea na masomo na Elimu Changamani (IPPE) ambayo inawahusisha vijana 112 waliomaliza elimu ya msingi na kukosa nafasi ya kujiunga na sekondari ambao hujengewa uwezo katika masomo ya maarifa, ufundi, afya, maktaba na mazingira.  
Kuhusu  maadhimisho ya mwaka huu Bw. Mecki Sadiki ameeleza kuwa pamoja na mambo mengine yatakuwa na mchango mkubwa katika kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu kusikiliza, kusoma na kutoa maoni ya upatikanaji wa katiba mpya nchini, kuongeza mwamko kwa jamii katika masuala ya elimu, kutathmini utekelezaji wa azimio la ulimwengu kuhusu utoaji wa elimu kwa wote na kutathmini mafanikio na mapungufu ya utekelezaji wa Elimu ya Watu Wazima (EWW) na Elimu Nje ya Mfumo Rasmi (ENMRA).

Comments

Popular posts from this blog