as cannes yamwagia sifa kapombe

kapombe2 1579f
Shomari Kapombe akitambulishwa rasmi AS Cannes
RASMI, klabu ya Daraja la Nne Ufaransa, AS Cannes imetangaza katika tovuti yake kwamba katika kujiimarisha ili kutoka katika kipindi kigumu, imeboresha kikosi chake kwa kumsajili kiungo Mtanzania, Shomari Salum Kapombe. (HM)

Klabu hiyo imesema hiyo pia itakuwa fursa kwa mchezaji huyo kutoka Simba SC ya Tanzania kujipatia uzoefu wa kimataifa akiwa na Weupe hao Ufaransa.
Imemuelezea Kapombe, kama kinda mwenye umri wa miaka 21, ambaye hadi sasa amekwishachezea mechi 14 timu yake ya taifa, Taifa Stars pamoja na kumkabidhi jezi kuanza rasmi mazoezi na wenzake.
Na imevutiwa naye zaidi baada ya wasifu wake kusema anaweza kucheza nafasi nyingine pia, zikiwemo za ulinzi, hivyo atakuwa msaada mkubwa kwa kocha Jean-Marc Pilorget msimu huu.
Imesema viongozi wanafanya jitihada kubwa kuhakikisha wanainua kiwango chake haraka ili aweze kufanikiwa zaidi Ulaya.
Wiki iliyopita, Simba SC ilitangaza kumuunganisha Kapombe na AS Cannes kwa mkataba wa maridhiano maalum.
Mwenyekiti wa Simba SC, Alhaj Ismail Aden Rage, alisema kwamba katika mkataba huo mpya na wa aina yake kuwahi kufanywa na klabu yoyote ya Tanzania, Simba imekubali mchezaji huyo achezee timu hiyo iliyo katika ligi daraja la nne la Ufaransa kwa makubaliano ya kumtafutia timu ya kucheza ndani ya miaka miwili kutoka sasa.
Rage amesema timu hiyo itamgharimia Kapombe kwa kila kitu wakati atakapokuwa nchini Ufaransa na endapo atauzwa kwenda katika timu nyingine yoyote, Simba itapata gawio lake kupitia mauzo hayo na lengo la mchezaji huyo kubaki Ufaransa ni pia kumtengeneza awe bora zaidi kuliko alivyo sasa.
Rage alisema katika mkataba huo mpya wa Kapombe, Simba imeangalia zaidi maslahi ya taifa na ya mchezaji kuliko ya klabu kwa vile kama mchezaji huyo atapata nafasi Ulaya, hilo litafungua milango kwa wachezaji wengi wa Kitanzania ambao kwa sasa hawapati fursa Ulaya.
Wakala wa Kapombe, Denis Kadito, alisema ingawa Kapombe ameonekana kuwa mchezaji mzuri, kutofahamika kwa jina la Tanzania kumekuwa kikwazo kikubwa kwa kupata kwake nafasi ya moja kwa moja na ndiyo maana.
Miongoni mwa nyota maarufu wa Ufaransa waliowahi kupita katika klabu hiyo ni Patrick Vieira, Zinedine Zidane na Luis Hernandez.
Klabu hiyo inafahamika kwa kuwa na miundombinu imara ya kumwezesha mwanasoka kijana kukuza uwezo wake na ni matarajio ya Simba Sports Club, Kadito, Cannes na Kapombe mwenyewe kwamba atakuwa mchezaji bora zaidi kuliko sasa katika kipindi cha mwaka mmoja kutoka sasa.
Kutokana na mkataba huo wa Kapombe na Cannes, Simba sasa imeongeza mkataba wake na mchezaji huyo kwa muda wa miaka mitatu zaidi, kwa vile mkataba wake wa sasa unamalizika Aprili mwakani.
Kama Kapombe hatafanikiwa kupata timu katika kipindi cha miaka miwili kutoka sasa, atarejea katika klabu ya Simba kuendelea na majukumu yake. Chanzo: binzubeiry

Comments

Popular posts from this blog